MAVUNDE AIPONGEZA OSHA KWA KUBORESHA UTENDAJI WAKE


Wafanyakazi waliokingwa ipasavyo wakifanya kazi za ujenzi katika mradi wa reli ya kisasa kutoka Dar es Salaam hadi Morogoro katika awamu ya kwanza ya mradi huo. OSHA huhakikisha kwamba wafanyakazi wanafanya kazi zao katika mazingira salama

****

Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu-Kazi, Vijana, Ajira na Watu Wenye Ulemavu, Mh. Antony Mavunde, ameupongeza Wakala wa Usalama na Afya Mahali pa Kazi (OSHA) kwa jitihada unazozichukua katika kuimarisha hali ya usalama na afya katika sehemu za kazi nchini.

Mh. Mavunde alizitoa pongezi hizo alipozungumza na wafanyakazi wa OSHA katika kikao cha pili cha baraza la tatu la watumishi hao kilichofanyika jijini Arusha mwishoni mwa wiki.

“Niwapongezi kwa kazi nzuri mnayoifanya katika kuboresha hali ya usalama na afya katika maeneo ya kazi hapa nchini. Kwakweli kumekuwa na mabadiliko makubwa sana katika utendaji wenu hasa katika kipindi cha hivi karibuni,” alisema Mh. Mavunde.

Aliongeza: “Kipindi cha nyuma mlikuwa mnafanya kazi zenu kama askari polisi jambo ambalo lilikuwa linawapa hofu kubwa wadau wenu ambao badala ya kuuelewa wajibu wao kisheria na kuutekeleza, waliishia kuwakwepa na kuwalalamikia.”

Kiongozi huyo wa serikali alieleza kwamba kwasasa watumishi wa OSHA wamekuwa wakijitahidi kufanya kazi kwa weledi mkubwa ikiwemo kuwaelimisha wadau ili waweze kuutambua wajibu wao kisheria na kuutekeleza bila kushurutishwa.

Kwa upande wake Mgeni Rasmi katika kikao hicho ambaye pia ni Katibu Mkuu (Ofisi ya Waziri Mkuu-Kazi, Vijana, Ajira na Watu Wenye Ulemavu), Eric Shitindi, aliwataka watumishi wa OSHA kuendelea kutekeleza majukumu yao katika namna ambayo itaboresha zaidi huduma kwa wanufaika wake.

“Kipindi cha nyuma kulikuwa na malalamiko mengi sana kutoka kwa watu tunaowahudumia lakini kwasasa malalamiko yamepungua sana. Hivyo nawaomba muendelee kutoa huduma nzuri kwa wateja wenu kwa kuzingia vyema Sheria na Kanuni mbali mbali zilizopo,” alisema mgeni rasmi.

Kaimu Mtendaji Mkuu wa Wakala, Khadija Mwenda, alisema kikao hicho cha baraza la wafanyakazi kinalenga kufanya tathmini ya utendaji wa taasisi kwa kipindi kilichopita na kuweka mikakati ya kujiimarisha zaidi kiutendaji kwa kipindi kijacho.


Wakala wa Usalama na Afya Mahali pa Kazi (OSHA) ni taasisi ya serikali yenye dhamana ya kusimamia masuala ya Usalama na Afya za wafanyakazi wanapokuwa katika sehemu zao za kazi. Wakala hufanya kaguzi za kiusalama na afya katika sehemu zote za kazi hapa nchini. OSHA pia huwashauri wamiliki ama wasimamizi wa maeneo ya kazi juu ya uwekaji na usimamizi wa mifumo ya kulinda afya na usalama wa wafanyakazi wanapokuwa kazini.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527