MBUNGE WA SINGIDA MAGHARIBI KINGU AMPIGA DONGO KIAINA TUNDU LISSU

Mbunge wa Singida Magharibi Elibariki Kingu amewaahidi wananchi wa Kata ya Siuyu jimbo la Singida Mashariki kuwa endapo watamchagua mgombea udiwani wa CCM, atakuwa mlezi wao na kwenda kuwasemea bungeni kuhusu matatizo ya maji waliyonayo, jukumu ambalo linapaswa kufanywa na Lissu ambaye ndiye mbunge wa hapo.

Mh. Kingu ametoa ahadi hiyo wakati akimnadi mgombea wa Udiwani kata ya Siuyu Wilayani Ikungi Mkoani Singida ambapo mbali na kuahidi kuwa mlezi wa kata hiyo amewaahidi akina mama kuwapatia Milioni 15 katika mfuko wa VICOBA endapo watafanikisha kumpatia ushindi mgombea huyo wa CCM Mgonto Juma Ramadhani

"Mimi kama Mbunge wa Singida Magharibi naahidi na nitayatekeleza baada ya uchaguzi wa tarehe 26. Nitatoa milioni 15 kwa ajili ya kata ya Siuyu peke yake na Ofisi za chama mmesema kwamba hamna viti nitawapatia Milioni moja kwa ajili ya viti. Nimepewa taarifa kuna vijiji havina maji hii agenda ya Siuyu nitaibeba na nitaipeleka Dodoma kuiwasilisha na baada ya hapo nitamleta Waziri wa Maji kuja kutatua hiyo changamoto", amesema Kingu

'Nimeogopa kuja na hizo fedha hapa kwa sababu watasema nahonga hivyo nitasubiri mpaka uchaguzi upite ndiyo nilete ili nisije kuchafua hali ya hewa kwa sasa" Kingu.

Kwa upande wa Mgombea wa Kata hiyo amewaomba wananchi kumchagua ili aende kuwawakilisha katika baraza la madiwani katika kutatua tatizo la maji ambalo lipo kwa mda mrefu na tatizo la barabara ambayo ni mbovu.

Uchaguzi katika kata ya Siuyu unafanyika baada ya Diwani Gerald Mahami aliyekuwepo kutoka (CHADEMA) kuvuliwa udiwani kutokana na kuwepo madai ya kushindwa kuhudhuria vikao vya baraza la madiwani.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527