RAIS MAGUFULI ATUMA SALAMU ZA RAMBIRAMBI VIFO VYA WATU 12 ZIWA VICTORIA

“Kwa mshtuko na masikitiko makubwa nimepokea taarifa ya vifo vya watu 12 waliopoteza maisha baada ya gari la abiria walilokuwa wakisafiria kutumbukia katika ziwa Victoria Mkoani Mwanza, nawapa pole sana wote waliopoteza jamaa zao katika ajali hii, nawaomba wawe na moyo wa uvumilivu, ustahimilivu na subira katika kipindi hiki cha majonzi”


Hiyo ni sehemu ya salamu za rambirambi alizozitoa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli kwa Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Bw. John Mongella kufuatia ajali ya basi la abiria (Daladala) lililozama katika ziwa Victoria baada ya kugonga vizuizi vya kivuko cha Kigongo Wilayani Misungwi na kisha kutumbukia na kuzama majini.


Mhe. Rais Magufuli amemtuma Bw. Mongella kufikisha salamu zake za pole kwa familia, ndugu, jamaa na marafiki wote waliopatwa na msiba huu na amesema anaungana nao katika maombolezo.


Aidha, Mhe. Rais Magufuli amewaombea marehemu wote wapumzishwe mahali pema peponi na majeruhi 3 walionusurika katika ajali hii wapone haraka ili waweze kuendelea na shughuli zao za kila siku.


Gerson Msigwa
Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, IKULU
Dar es Salaam

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post