FAMILIA YA TUNDU LISSU YATOA MSIMAMO MPYA

Familia ya Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu leo imefunguka na kutoa msimamo wake kuhusu jeshi la polisi na kusema hawaoni jitihada zozote kutoka kwenye jeshi hilo kuchunguza jaribio la mauaji ambalo ndugu yao lilimpata Septemba 7, 2017. 

Mdogo wa Tundu Lissu ambaye anafahamika kwa jina la Vicenti Mughwai Lissu akiongea na waandishi wa habari amesema kuwa wanaona jeshi la polisi halipo 'serious' katika kufanya uchunguzi juu ya shambulio la Lissu. 

"Kwa jinsi ambavyo ndugu yetu anamchango mkubwa kwa hili taifa, hata kama yupo upande wa pili lakini sisi tunaona zoezi hili la uchunguzi haliendi vizuri, hivyo tunaona kuna haja sasa labda ya kushirikisha wapelelezi kutoka nje ya nchi ambao wako wengi tu kwa sababu nia si njema, tunakataka kujua nani amefanya hili tukio si ndiyo basi washirikiane na wataalam wa nje kama ambavyo walifanya kwenye kulipuliwa kwa ubalozi wetu ili waweze kupatikana kwa sababu kwenye mitandao huko wengine wanasema CHADEMA wanauana wao kwa wao, wengine wanasema upande wa pili sasa sisi tunasema uchunguzi ufanyike ili ukweli uwe wazi" alisema Vicenti Lissu 

Aidha familia hiyo imelitaka jeshi la polisi kufanya uchunguzi haraka juu ya sakata la ndugu yao kupigwa risasi na pia wamewaomba Watanzania waendelee kumuombea Tundu Lissu ili aweze kupona. 

Mbunge Tundu Lissu alipigwa risasi na watu wasiojulikana mnamo Septemba 7, 2017 akiwa mjini Dodoma na baadaye kupelekwa Nairobi nchini Kenya kwa matibabu zaidi ambapo mpaka sasa yuko huko kwa matibabu.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post