WABUNGE WA UPINZANI WAGOMA TENA..WATOKA BUNGENI

Mapema leo Septemba 12, 2017 umetokea mgomo mwingine Bungeni kutoka kwa wabunge wa upinzani wakigomea kuapishwa kwa wabunge wateule wa Chama cha Wananchi CUF.


Huu unakuwa ni mwendelezo wa mgomo ule wa awali Septemba, 5 mwaka huu ambapo wabunge wa upinzani walitoka nje ya ukumbi wa bunge wakieleza kutounga mkono kitendo cha kuapishwa kwa wabunge Saba wa CUF.


Wabunge wa Upinzani hususani wale wanaotoka vyama vinavyounda Ukawa wametoka nje ya Ukumbi wa Bunge leo wakipinga kuapishwa kwa mbunge mmoja wa CUF upande wa Lipumba aliyekuwa amebaki kati ya wale Saba walioapishwa Septemba 5 mwaka huu.


Mbunge wa Viti Maalum CHADEMA Suzan Lyimo amesema wameamua kutoka nje baada ya kuona 'Order Paper' ikionyesha kuna Mbunge wa CUF anaapishwa.Lyimo amesema wataendelea kususia tukio lolote linalohusisha wabunge hao wapya wa CUF.


Kumekuwepo na mgogoro ndani ya CUF hali iliyopelekea kuwepo kwa makundi mawili moja likiwa ni kundi linalilomuunga mkono Mwenyekiti wa CUF anayetambuliwa na Msajili wa vyama vya siasa Profesa Lipumba, huku kundi lingine likiwa ni upande wa Katibu Mkuu wa CUF taifa Maalim Seif.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527