MKURUGENZI WA TANESCO ALIMWA BARUA YA KUJIELEZA

Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Dk Medard Kalemani amemtaka Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco), Dk Tito Mwinuka kuandika barua kujieleza ni kwa nini ameshindwa kuanza ujenzi wa kituo cha kupoozea umeme cha Kigamboni.


Dk Kalemani ametoa agizo hilo baada ya kutembelea vituo vya kupoozea umeme vya Gongo la Mboto, Kurasini na Kigamboni.


Mwezi uliopita naibu waziri alimwagiza Dk Mwinuka kuanza ujenzi haraka lakini baada ya kutembelea jana Jumatatu amekuta eneo hilo bado halijafanyiwa usafi.


“Nataka kesho( leo) nipate taarifa ya maandishi ni kwa nini hadi sasa hujaanza ujenzi wa kituo cha kupoozea umeme cha Kigamboni licha ya kukuagiza uanze ujenzi,” aliagiza.


Dk Kalemani alisema Agosti alitembelea eneo hilo na kumuagiza mkurugenzi kujenga uzio ili watu wasivamie eneo hilo.


Alisema pia, alimuagiza kuanza ujenzi wa kituo cha kupoozea umeme kwa sababu Sh5 bilioni zimeshatengwa kwa kazi hiyo.


“Nashangaa sasa ni mwezi mmoja lakini hakuna kilichofanyika, umeshindwa hata kufyeka majani ili kuonyesha kuna mradi utafanyika hapa,” alihoji Dk Kalemani.


Naibu waziri aliagiza makandarasi kwenye vituo vya kupoozea umeme kumaliza kazi kwa wakati ili kuondoa matatizo ya umeme kwa wakazi wa Mbagala, Kigamboni na Gongo la Mboto.


“Sitalala nitakuwa natembelea miradi hii kila mara hadi itakapokamilika,” alisema.


Akizungumzia agizo hilo, Dk Mwinuka alisema tangu naibu waziri alipolitoa wamekuwa wakifuatilia kibali cha athari za mazingira ambacho hutolewa na Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (Nemc).


“Tukipata kibali tutaanza ujenzi mara moja na tunakuahidi kazi hiyo itamalizika kwa muda uliopangwa Machi mwakani.


Mbunge wa Kigamboni, Dk Faustine Ndugulile alisema kuchelewa kukamilika kwa vituo vya kupoozea na kusambaza umeme kunasababisha matatizo ya nishati isiyo ya uhakika katika jimbo hilo.


Mkuu wa Wilaya ya Kigamboni, Hashim Mgandilwa alisema mradi huo ukianza atausimamia kwa kuwa tatizo la umeme linaathiri maendeleo na uchumi.


“Kila siku napokea ujumbe wa maandishi wa simu kunijulisha tatizo la umeme, ni aibu kwa kuwa wakati mwingine nashindwa nijibu nini,” alisema.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527