JAJI MKUU : MAHAKAMA HAIJAMSUSA TUNDU LISSU


SIKU 15 baada ya Mbunge wa Singida Mashariki na Rais wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS), Tundu Lissu kupigwa risasi na watu wasiojulikana, Jaji Mkuu wa Tanzania, Profesa Ibrahim Juma amesema, mahakama haijalifumbia macho tukio hilo kwa kuwa ni jambo ambalo litafikishwa mahakani.

Jaji Juma amesema kwa mujibu wa kanuni jambo litakalofikishwa mahakamani kwa ajili ya kutolewa ushahidi halipaswi kuongelewa au kutolewa maoni na kwamba tukio hilo la Lissu litafikishwa mahakamani baada ya taratibu zote kukamilika.

Profesa Ibrahim Juma ameyasema hayo jana wakati akizungumza na wanahabari katika Mahakama ya Rufaa, ambapo apia amewataka wananchi wenye ushahidi unaohusiana na tukio hilo kuwasilisha katika mamlaka husika badala ya kusambaza mitandaoni.

“Sisi mahakama kanuni zetu haturuhusiwi kutoa maoni au kuongelea jambo ambalo tunaona moja kwa moja litakuja mahakamani, kanuni zetu ziko wazi. Na ndio maana mnatuona kimya, kwenye mitandao mnajaribu kutuvuta tutoe maoni, hatutasema,” amesema Jaji Juma.

Amesema tamko lililolewa na Chama cha Wanasheria wa Marekani kulaani tukio hilo ni la kawaida linalowahimiza wanaokusanya ushahidi wafanye kazi yao kwa haraka na kupeleka mahakamani na kwamba kazi ya mahakama ni kuangalia ushahidi na kutoa uamuzi.

IMEANDIKWA NA KATUMA MASAMBA- habarileo

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527