KAULI YA JESHI LA POLISI KUHUSU OFISI ZA MAWAKILI IMMMA ADVOCATES KULIPULIWA DAR

Jeshi la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, leo limesema kuwa uchunguzi wa awali umebaini kuwa watu wasiojulikana utambulisho wao na idadi yao walifika katika ofisi za Mawakili wa IMMMA Advocates wakiwa katika magari mawili na kujifanya ni maaskari na kuwarubuni walinzi na kuondoka nao katika gari mojawapo kabla ya kulipua jengo hilo.


Walinzi hao wanadaiwa kukutwa baadaye maeneo ya Kawe wakiwa hawajitambui.


Imedaiwa kuwa kundi lililobaki liliingia katika ofisi hizo hilo na kuweka vilipuzi vilivyotengenezwa kienyeji, ambavyo vililipuka muda mfupi baada ya watu hao kuondoka eneo hilo na kusababisha uharibifu wa wa mali na jengo la ofisi hiyo pamoja na majengo ya jirani.


Jeshi hilo limesema kuwa linaendelea kufanya uchunguzi wa kina ili kubaini watu waliofanya tukio hilo na kujua dhamira yao ili wafikishwe katika vyombo vya sheria kwani wajibu wa jeshi la polisi ni kulinda raia na mali zao na kamwe haliwezi kuhujumu maisha ya watu na mali za wananchi


Aidha, jeshi hilo limewaomba waathirika wa tukio hilo na wananchi kwa ujumla kuwa watulivu wakati vyombo vya dola vikiendelea na upelelezi wa tukio hilo

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527