HARBINDER SETHI WA ESCROW KAWEKEWA MAPUTO TUMBONI...YANAWEZA KUPASUKA AKAFARIKI

Wakili wa mshtakiwa Harbinder Sethi, Joseph Makandege ameulalamikia upande wa Jamhuri kwa kushindwa kumpeleka mteja wake Hospitali ya Taifa Muhimbili kama Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, ilivyoamuru.

Amedai hali hiyo inahatarisha afya ya mteja wake kwani akikosa kupata matibabu sahihi anaweza kupoteza maisha kutokana upasuaji aliofanyiwa uliosababisha kuwekewa maputo tumboni.

“Mara mbili mahakama ilitoa amri ikielekeza utawala wa Magereza kumpeleka mshtakiwa wa kwanza Muhimbili , amri ilitolewa baada ya mahakama kukubaliana na hoja za upande wa utetezi, lakini badala ya kumpeleka Muhimbili, Magereza walimpeleka mshtakiwa Hospitali ya Amana.

“Kwa taarifa za kitabibu ni kwamba hali ya mshtakiwa wa kwanza isipohudumiwa ipaswavyo inaweza kusababisha kifo kwani maputo yanaweza kupasuka tumboni , mahakama iliekeza mshtakiwa apelekwe moja kwa moja Muhimbili ambayo ni hospitali ya juu kabisa ya Serikali, ndio nategemea inaweza kuwa na wataalamu na vifaa thabiti kwa ajili ya matatizo yanayomkabili mshtakiwa wa kwanza,” amedai.

Makandege alidai amri zote zilizotolewa na mahakama hazijatekelezwa , aliomba mahakama itoe amri nyingine ya kuutaka upande wa Jamhuri kuamuru amri iliyotolewa itekelezwe.

Akijibu Wakili wa Serikali Mkuu, Vitalis Peter amedai Jamhuri haijakaidi amri ya mahakama na kwamba Magereza wana utaratibu wao ambapo wanahojiana na mgonjwa wakiona tatizo lake hawana utaalamu nalo wanampa rufaa kwenda Muhimbili. Kesi hiyo imeahirishwa hadi Septemba 14 mwaka huu kwa ajili ya kutajwa.

Washtakiwa katika kesi hiyo mshtakiwa Seth na James Rugemarila, wanakabiliwa na kesi ya uhujumu uchumi ikiwa na mashitaka 12 yakiwemo ya kutakatisha fedha hivyo kuwafanya wakose dhamana.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527