VICHWA VYA WATU VYAPATIKANA KWENYE KABURI MOJA,VINNE VYAKUTWA NDANI YA FRIJI


Maafisa Mexico wamefukua miili 32 na vichwa tisa vya watu kutoka kwa kaburi la pamoja kusini mwa nchi hiyo katika eneo lililoathiriwa sana na mauaji ya magenge ya walanguzi wa mihadarati.

Wachunguzi wa jinai walifukua miili 31 ya wanaume na mmoja wa mwanamke katika eneo la milimani la Zitlala, ambapo makabiliano kati ya magenge ni jambo la kawaida.

Msemaji wa maafisa wa usalama amesema wanaendelea kuchunguza iwapo kuna miili zaidi.

Hakuna aliyekamatwa kuhusiana na mauaji hayo.

Miili hiyo ilipatikana katika mashimo 17 tofauti karibu na kijiji cha Pochahuixco kati ya Jumanne na Alhamisi.

Msemaji wa maafisa wa usalama Roberto Alvarez ameambia shirika la habari la AFP kwamba makaburi hayo yaligunduliwa 
baada yao kupashwa habari na wadokezi.

AFP imeripoti kwamba vichwa vinne vilipatikana "ndani ya friji".

Mji huo unapatikana katika jimbo la Guerrero mauaji hutokea mara kwa mara. Watu zaidi ya 1,800 wameuawa eneo hilo kati ya Januari na Oktoba mwaka huu.

Chanzo-BBC Swahili

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527