MAKADA WA CHAMA CHA KIKOMUNISTI CHA CHINA (CPC) WAANZA ZIARA TANZANIA KUJIFUNZA MAMBO YA CCM


UJUMBE wa watu sita kutoka Chama cha Kikomunisti cha China (CPC) uko nchini kwa ziara ya siku saba kujifunza shughuli zinazofanywa na CCM.


Akizungumza na waandishi wa habari jana, Mwenyekiti wa CCM wa Mkoa wa Dar es Salaam, Ramadhani Madabida alisema ujumbe huo unaongozwa na Mkurugenzi wa Idara ya Uhusiano wa Kimataifa, Maendeleo na Mafunzo wa Chuo cha Viongozi wa Chama hicho, Jia Bo.


Madabida alisema lengo la ziara hiyo ni kudumisha ushirikiano baina ya Tanzania na China ulioasisiwa na marehemu Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere na Baba wa Taifa la China, marehemu Mao Tse-Tung.


Alisema ujumbe huo ambao utatembelea Temeke na Zanzibar uliwasili nchini baada ya ziara ya baadhi ya makada wa CCM waliokwenda China na kujifunza mambo mbalimbali ambayo ujumbe huo utapenda kujua kama wameyafanyia kazi.


Mratibu wa Masuala ya Siasa na Uhusiano wa Kimataifa wa CCM, Dk Pindi Chana alisema ujio wa viongozi wa chama hicho ni matunda ya ushirikiano wa Tanzania na nchi mbalimbali duniani.


"Ujio wa wenzetu hawa kutoka China ni matunda ya ushirikiano kati yetu na nchi zingine kama Zimbabwe, Afrika Kusini, Angola, Cuba na zinginje za Ulaya hasa katika siasa za kijamaa," alisema Chana.


Alisema China wako karibu bilioni moja na wamepiga hatua katika maeneo mbalimbali hivyo ujio wao nchini ni fursa kwao kujifunza mambo yetu na sisi kujifunza kwao kutokana na hatua ya kiuchumi waliyopiga..

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527