WANNE WANASWA WAKIWA NA MAGAMBA YA KAKAKUONA YENYE THAMANI YA ZAIDI YA BILIONI 1.4

Kakakuona


WATU wanne wakiwemo raia watatu wa Burundi, wanashikiliwa na Polisi mkoani Morogoro baada ya kukutwa na magamba ya kakakuona, yenye thamani ya zaidi ya Sh bilioni 1.4.

Walikuwa wamehifadhi magamba hayo kwenye mifuko 67, yakisubiri kusafirishwa kwenda nje ya nchi kuuzwa. Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Morogoro, Ulrich Matei, alisema watu hao walikamatwa saa tano na nusu usiku wa Oktoba 28, mwaka huu eneo la mtaa wa Reli, kata ya Kichangani, Manispaa ya Morogoro.

Walinaswa ndani ya ghala moja, lenye mashine ya kukoboa na kusaga nafaka.

Alisema, askari wa jeshi hilo wakiwa katika msako, walipokea taarifa za kiintelejensia kutoka kwa raia wema kuhusu mazingira ya watu katika eneo hilo. Walipofika, walikuta watuhumiwa hao wanne.

Baada ya upekuzi kwenye ghala hilo, polisi walikamata magamba ya kakakuona katika mifuko 67, baaadhi yake yakiwa tayari kwa ajili ya kusafirishwa kwenda nje ya nchi.

Kamanda Matei aliwataja raia wa Burundi waliokamatwa kuwa ni Kibonese Golagoza ( 35), Nuru Athuman (32) na Benjamin Gregory Luvunduka (41) ambao pia ni wakazi wa Morogoro, wakati Mtanzania ni Shukuru Mwakalebela (25) mkazi wa Stesheni mjini hapa.

Alisema magamba hayo, yalifungwa katika mifuko yenye kilo 50 na kisha kutumbukizwa kwenye viroba vikubwa vya kilo 100, vilivyochanganywa na maharage. Aidha alisema watuhumiwa raia wa Burundi, wanakabiliwa pia na tuhuma za kuingia nchini bila kibali cha Uhamiaji.

Alisema wote wanaendelea kuhojiwa na Polisi na watafikishwa mahakamani upelelezi utakapokamilika. Hata hivyo, Kamanda huyo alisema ni mapema kueleza kakakuona hao wanauawa katika maeneo gani ya nchi, na mahali liliko soko kubwa kwa vile suala hilo lipo katika uchunguzi na utakapokamilika, taarifa itatolewa.

Ofisa Maliasili wa Mkoa wa Morogoro, Joseph Chuwa aliyekuwepo katika upekuzi huo, alisema katika mifuko 67 iliyokamatwa, kila mmoja ulikuwa na wastani wa magamba ya kakakuona 1,000.

Alisema kakakuona mmoja, kwa wastani anakuwa na magamba 60 hadi 100, hatua iliyofanya kila mfuko kuwa na wastani wa kakakuona wapatao 10 waliouawa kwa ajili ya biashara hiyo haramu.

Alisema kutokana na idadi ya mifuko hiyo, wastani wa kakakuona 670 waliuawa, ambapo kilo moja ya magamba yake huuzwa kwa dola za Marekani 960, hivyo kutokana na viwango vya sasa vya thamani ya dola kwa fedha ya Tanzania, ni sawa na Sh bilioni 1.4.

Chuwa alisema kutokana na wingi wa magamba hayo ya kakakuona, ujangili huo hauwezi kuwa umefanyika mkoani Morogoro pekee, bali pia katika maeneo mengine ya hapa nchini, kwa kuwa kiwango hicho ni kikubwa na hayakupatikana kwa wakati mmoja. Alisema soko kubwa la bidhaa hiyo ni katika Bara la Asia.

Kakakuona kwa ufupi

Kakakuona ndiye mnyama pekee duniani, ambaye mwili wake wote umefunikwa na magamba makubwa kuliko ya viumbe wengine. Hutumia magamba hayo, kama silaha ya kujilinda dhidi ya maadui. Jina la kakakuona lilianzia nchi za Mashariki ya Mbali za Malaysia, Indonesia na Brunei, likimaanisha kitu kinachojikunja.

Kwa kawaida, Kakakuona hupenda kujikunja kama mpira. Hiyo ni mbinu anayotumia kujilinda dhidi ya maadui. Kakakuona akiona adui, hujilinda kwa kujikunja, lakini akiona hali inakuwa mbaya zaidi, hutema sumu kali mithili ya tindikali inayoweza kumdhuru adui.

Pia, wakati mwingine hunyoosha mkia wake na kuuzungusha na kumkamata adui aliyekaribu yake. Licha ya kutumia mbinu hiyo kujilinda, lakini anapojikunja ndiyo inakuwa rahisi kwa watu kumkamata na kumbeba. Kuna aina nane za kakakuona duniani, zilizopo duniani kwa zaidi ya miaka milioni 80 ya mabadiliko yao.

Kati ya hizo, aina nne zinapatikana Bara la Ulaya na nyingine barani Afrika. Kakakuona ana ulimi wenye urefu unaozidi mwili wake. Akiurefusha kwa kuutoa nje ya kinywa, unafikia urefu wa sentimita 40. Ulimi huo ambao pia unanata, huutumia kwa ajili ya kukusanya wadudu, ambao ndiyo mlo wake wa pekee.

Hana mlo mwingine zaidi ya huo kutokana na kukosa meno. Baadhi ya kakakuona huishi juu ya miti. Wengine hujichimbia ardhini na kuishi ndani ya mashimo. Wanaoishi juu ya miti ni wenye mikia mirefu wanaopatikana barani Afrika. Wengine huchimba mashimo marefu ardhini na kuishi humo ili wasikutane na binadamu.

Inakadiriwa kuwa kakakuona 100,000 hukamatwa kila mwaka barani Afrika na Ulaya na kuuzwa. China na Vietnam ndizo nchi maarufu ambazo nyama na magamba yake huuzwa. Inakadiriwa kuwa mamilioni ya wanyama hao, wameuawa na kuuzwa katika miaka 10 iliyopita.

Chanzo-Habarileo

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527