Tanzia: BONDIA MAARUFU TANZANIA THOMAS MASHALI AUAWA DAR


HABARI zilizotufikia hivi punde zinasema kuwa Bondia mahiri na machachari ulingoni, Thomas Mashalli, almaarufu 'Simba asiyefugika', amefariki dunia usiku wa kuamkia leo huko maeneo ya Kimara baada ya kupigwa na watu wasiojulikana.




Imeelezwa kuwa bondia huyo alifika maeneo ya Kimara katika moja ya baa na kuanza kunywa bia na baadaye ukazuka ugomvi baina yake na kijana mmoja aliyekuwa maeneo hayo jambo lililofamfanya bondia huyo kumwadhibu kijana huyo kwa kumchapa mangumi. 



Baada ya ugomvi huo, imeelezwa kuwa kijana huyo alianza kupiga kelele huku akimuitia mwizi bondia huyo, jambo lililowafanya watu wasioujua ukweli wa tukio hilo kufika eneo hilo na kuanza kumshambulia bondia huyo kwa silaha mbalimbali zikiwemo mapanga. 



Baada ya watu hao kumjeruhi imeelezwa kuwa waliamua kumburuza hadi barabarani na kumtupa na kisha kumwacha akiugulia maumivu.


Akizungumza na mtandao huu,Promota wake Kaike Siraju, amethibitisha  kufariki kwa bondia huyo aliyekuwa apande uliongoni mwezi ujao huko mjini Morogoro. 



Msiba wa bondia huyo upo maeneo ya Tandale nyumbani kwa wazazi wake. 

Bwana alitoa na bwana ametwaa, jina lake lihimidiwe
Mungu ilaze roho ya marehemu mashali, mahala pema peponi. Amina 



TUTAENDELEA KUWAJUZA KADRI HABARI ZITAKAVYOTUFIKIA.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527