Kumekucha Stand United!! Kamati ya Uchaguzi Yapitisha Majina 12 Ya Wagombea Wa Nafasi za Uongozi


 
Hatimaye kamati ya uchaguzi ya Klabu ya Stand United (CHAMA LA WANA) ya mjini Shinyanga imepitisha majina 12 ya wagombea wa nafasi za uongozi wa ngazi mbalimbali ndani ya klabu hiyo baada ya kuomba na kufanyiwa usaili,anaripoti
Stephen Mwita-Malunde1 blog Shinyanga.



Katika taarifa yake kwa vyombo vya habari mwenyekiti wa kamati ya uchaguzi ya klabu hiyo itakayodumu kwa muda wa miaka miwili wakili wa kujitegemea Paul Kaunda amesema fomu za kugombea uongozi zilitolewa tangu June 14 hadi 17 mwaka huu ambapo waliojitokeza kuzichukua walikuwa ni 14 na jana (June 19,2016) walifanyiwa usaili.

Amewataja waliopitishwa kugombea baada ya usaili huo kuwa ni Emmanuel Kaombe, Dkt. Ellyson Maeja, Ibrahim Mbogo na Salum Kitumbo kwa nafasi ya Uenyekiti wakati nafasi ya Makamu mwenyekiti ikigombewa na Luhende Luhende.

Katika nafasi ya wajumbe wa kamati ya utendaji ndani ya Klabu hiyo wakili Kaunda amewataja waliopitishwa na kamati yake kuwa ni pamoja na Twahil Njoki, Geofrey Tibakyenda, Stephan Mihambo , Jackline Burahi na Jimrod Tilweshobwa.

Wengine ni Francisco Magoti na Mariam Richard na kuwataja walioenguliwa kuwa ni mwanasiasa mkongwe aliyewahi kuwa katibu mwenezi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wilaya ya Shinyanga Mjini Charles Shigino na Abert Silwimba.

Uchaguzi mkuu wa viongozi ndani ya Klabu hiyo unatarajiwa kufanyika Jumapili ya Juni 26 mwaka huu baada ya Klabu hiyo kuongozwa na viongozi wa mpito tangu kuanzishwa kwake mwaka 2012 na kuisababishia migogoro kwa mipindi kirefu na Shirikisho la soka nchini (TFF) kuitaka kufanya uchaguzi wa kikatiba haraka iwezekanavyo.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post