WAGOMBEA 7 WA URAIS ZANZIBAR WAKABIDHIWA WALINZI

Jecha
Wagombea saba wa nafasi ya urais wa Zanzibar katika uchaguzi mkuu wa marudio wa Machi 20 wamekabidhiwa walinzi binafsi kutoka Jeshi la Polisi, imeelezwa.
 
Mgombea wa nane, Rais Ali Mohamed Shein ataendelea na ulinzi wake kutokana na wadhifa alionao.

Wagombea urais waliokabidhiwa walinzi ni Khamis Iddi Lila wa (ACT-Wazalendo), Juma Ali Khatib (TADEA), Soud Said Soud (AFP), Hamad Rashid Mohamed(ADC), Issa Mohamed Zonga(SAU), Hafidh Hassan Suleiman (TLP) na Ali Khatib Ali (CCK).

Taarifa hiyo ilitolewa na Mkurugenzi wa Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC), Salum Khasim Ali alipokuwa akitoa mwongozo wa Tume katika Kikao cha Viongozi wa Vyama na wagombea.

Alipoulizwa kuhusu mgombea wa chama chake kupewa ulinzi wakati walishatangaza kutokugombea kwenye uchaguzi huo, Mwenyekiti wa CCK, Constantine Akitanda, alisema hawatambui suala hilo.

“Kwa nini serikali itoe ulinzi wakati viongozi wa chama hatuna taarifa, ikuna kamati inashughulikia suala hilo na imeshakamilisha kazi ila sijapitia maelezo yao, nipo msibani,” alisema.

Wagombea ambao hawakuhudhuria katika Kikao hicho ni Mohamed Masoud Rashid wa CHAUMA, Seif Ali Iddi (NRA), Kassim Bakar Ali (Jahazi asilia), Abdalla Kombo Khamis (DP), Tabu Mussa Juma (D-Makini) na Maalim Seif Sharif Hamad (CUF) ambao wametangaza kujitoa katika uchaguzi huo.

Vyama sita hivyo vinapinga kufanyika uchaguzi wa marudio kwa madai kuwa Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 25 mwaka jana ulikuwa huru na wa haki.

Vyam hivyo vinanukuu ripoti za waangalizi wa uchaguzi wa ndani na je waliokuwepo visiwani hapa mwaka jana kushuhudia Uchaguzi Mkuu huo.

ZEC imesisitiza uchaguzi wa marudio utafanyka bila ya wagombea kufanya kampeni katika visiwa vya Ungunja na Pemba.

Licha ya vyama vingi kutangaza kujitoa katika uchaguzi huo, ZEC imesema karatasi za kupigia kura zitakuwa kama zilizotumika katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka jana.

Mgombea urais wa Jahazi Aslia, Ali alisema chama chake hakipo tayari kupokea matokeo yoyote kama tume imegoma kuondoa majina yao katika karatasi za kupigia kura.

Alisema hata kama ZEC watatangaza matokeo watakuwa wanafanya kazi ya kujifurahisha kwa sababu hawatoyatambua matokeo yake.

Alisema kuwa ni jambo la kusikitisha ZEC kuendelea kung'ang'ania wagombea walioamua kujiondoa katika uchaguzi wa marudio wakati kushiriki au kutoshiriki ni hiyari ya mgombea.

Naye Mkurugenzi wa Mawasiliano wa CUF, Hamad Masoud Hamad alisema ZEC lazima itambue uteuzi wa Septemba 6 mwaka jana wa wagombea, na kiapo walichokula mahakamani ilihusu Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 25 na si uchaguzi wa marudio wa Machi 20.

Hamad alisema wananchi na dunia inatambua kuwa CUF imejitoa katika uchaguzi wa marudio na hawatokuwa tayari kupokea matokeo yoyote ya uchaguzi huo.

Alisema ZEC inatakiwa kuheshimu maamuzi waliofanya wananchi Oktoba 25 mwaka jana na kukamilisha kufanya majumuhisho katika majibo 23 yaliyokuwa yamebakia kati ya 54 na kumtangaza mshindi wa urais katika uchaguzi huo.

Mgombea wa CUF, Hamad na wawakilisihi wa chama hicho walikuwa wakiongoza wakati ZEC ilipotangaza kufuta matokeo hayo ya Uchaguzi Mkuu wa Mwaka jana ambao pia ulitumika kuchagua Rais wa Jamhuri na Wabunge.

Alisema kuwa katiba ya Zanzibar hairuhusu kufanyika uchaguzi mara mbili ndani ya miaka mitano na hakuna kifungu cha katiba au sheria kinachompa uwezo mwenyekiti wa tume kufuta matokeo ya Uchaguzi Mkuu wa Zanzibar.

CHANZO: NIPASHE JUMAPILI

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527