RAIS MAGUFULI AWASILI ARUSHA KWA AJILI YA KUONGOZA MKUTANO WA WANACHAMA WA JUMUIYA YA AFRIKA MASHARIKI




Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli amewasili Mkoani Arusha ambako pamoja na mambo mengine ataongoza Mkutano wa 17 wa kawaida wa wakuu wa nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki utakaofanyika Jumatano tarehe 02 Machi, 2016 Mjini Arusha.


Katika uwanja wa ndege wa kimataifa wa Kilimanjaro (KIA) Rais Magufuli amelakiwa na viongozi mbalimbali wa vyama vya siasa na serikali pamoja na vikundi vya burudani za ngoma kabla ya kuelekea Arusha Mjini.


Rais Magufuli ndiye Mwenyekiti wa sasa wa Jumuiya ya Afrika Mashariki inayojumuisha nchi za Tanzania, Kenya, Uganda, Rwanda na Burundi.Kabla ya kuongoza kikao hicho Rais Magufuli anatarajiwa kukutana na kufanya mazungumzo ya ana kwa ana na viongozi wakuu wa nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki.


Tarehe 03 Machi, 2016 Rais Magufuli na Rais wa Jamhuri ya Kenya, wataweka jiwe la msingi katika mradi wa ujenzi wa barabara ya Arusha - Holili - Taveta - Voi inayoziunganisha nchi za Tanzania na Kenya.


Barabara hiyo ni sehemu ya miradi ya maendeleo ya Jumuiya ya Afrika Mashariki inayotekelezwa na nchi wanachama wa Jumuiya hiyo.


Gerson Msigwa
Kaimu Mkurugenzi wa Mawasiliano, IKULU.
Dar es Salaam
28 Februari 2016

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527