HII NDIYO BODI MPYA YA WAKURUGENZI TBC,YUMO DKT AYUBU RIOBA, BALOZI HERBERT MRANGO NDIYO MWENYEKITI

MKUTANO WA MHE. NAPE MOSSES NNAUYE, WAZIRI WA HABARI UTAMADUNI SANAA NA MICHEZO NA WAANDISHI WA HABARI



TAREHE 20/02/2016

-------------

Dondoo Alizozungumza Waziri Nape Nnauye;

Napenda kuwafahamisha kuwa kufuatia Bodi ya Wakurugenzi ya Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC) kumaliza Muda wake, uundwaji wa Bodi Mpya umekamilika.


Ni vyema kuwafahamisha kuwa katika utaratibu wa kisheria wa kuunda Bodi ya TBC mwenye Mamlaka ya kisheria ya Kumteua Mwenyekiti wa Bodi ni Rais wa Jamhuri ya Muugano wa Tanzania.



Napenda kutumia fursa hii kumshukuru sana aliyekuwa Mwenyekiti wa Bodi ya TBC iliyomaliza muda wake, Prof. Mwajabu Possi na wajumbe wake wote kwa kazi waliyoifanya kwa muda wote wa uhai wa bodi hiyo.


Ninaamini Bodi Mpya itaendeleza yale mazuri yote yaliyofanyika na Baodi iliyopita na kubuni mambo mengine mapya ili kuongeza tija kwa Shirika.


Baada ya kutoa maelezo haya ya awali, sasa nichukue fursa hii kuwajulisha yafuatayo;

1. Mhe. Dkt. John Pombe Joseph Magufuli amemteua Mhe. Balozi Herbert E. Mrango (pichani) kuwa Mwenyekiti Mpya wa Bodi ya TBC. Uteuzi huu unaanza tarehe 19/02/2016 kwa kipindi cha miaka Mitatu.


Balozi Mrango kielimu ana shahada ya Uzamili katika uendelezaji wa Mifumo (MSc – Systems Development) aliyoisomea Chuo Kikuu cha Dublin Nchini Uingereza. Aidha amehitimu Shahada ya kwanza ya Takwimu za Kiuchumi katika Chuo Kikuu Cha Dar Es Salaam, Tanzania.



Balozi Mrango alishashika nyadhifa mbalimbali, zikiwemo kuwa Katibu Mkuu wa iliyokuwa Wizara ya Miundombinu Kuanzia Februari, 2011 hadi September, 2013.



Nachukua fursa hii kumpongeza Mhe. Balozi Mrango kwa kuaminiwa na Mhe. Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania kushika wadhifa huu muhimu.





Aidha nimhakikishie Mwenyekiti huyu Mpya wa TBC kwamba kwa kuwa Shirika la TBC liko chini ya Wizara yangu, tutampa ushirikiano wa kutosha ili kuendelea kuleta mabadiliko chanya katika shirika letu la Utangazaji.





2.Kwa mujibu wa Sheria iliyounda TBC, baada ya Mhe. Rais kumteua Mwenyekiti wa Bodi, Waziri mwenye dhamana na shughuli za utangazaji, anateua Wajumbe sita wa Bodi.





Katika uteuzi wa wajumbe wa Bodi ya Shirika la Umma, Ofisi ya Msajili wa Hazina ilishatupatia vigezo vya utaalamu wa wajumbe wakati wa uteuzi.


Hivyo basi, mimi Nape Moses Nnauye, nikiwa Waziri wa Habari, Utamaduni Sanaa na Michezo, kwa kuzingatia vigezo vilivyobainishwa na Ofisi ya Msajili wa Hazina na kwa kufuata taratibu zingine za kufanya uteuzi, nimewateua wafuatao kuwa wajumbe wa Bodi ya TBC;


(i) Bw. William Steven Kallaghe; Mtaalamu wa Uchumi. (M.A – Economics; Head of Public Policy: NBC Bank Tanzania ).


(ii)Bw. Mustapha Kambona Ismail; Mtaalamu wa Sheria. (LLB - UDSM; Associate Director, Litigation & Investment – Bank of Tanzania; Advocate of the High Court of Tanzania).


(iii) Bi. Elimbora Abia Muro; Mtaalamu wa Uhasibu. (CPA, MBA: Senior Internal Auditor, Tanzania Investment Centre).


(iv) Bw. Mick Lutechura Kiliba; Mtaalamu wa Rasilimali watu. (MBA – Public Service Mgt; Director of Management: President’s Office – Public Service Management).


(v) Dkt. Ayub Rioba; Mtaalamu wa Sekta ya Utangazaji na Utangazaji. (PhD – Mass Communication; Associate Dean: School of Journalism, University of Dar Es Salaam) na

6. Bw. Assah Andrew Mwambene; Mtaalamu wa Sekta ya Habari. ( MSc – Media Research and Analysis; Director of Information: Ministry of Information, Culture, Arts and Sports).


Uteuzi wa wajumbe hawa ni kuanzia tarehe 19/02/2016 kwa muda wa miaka mitatu.

3. Nimalizie kwa kuwapongeza tena wote waliopata uteuzi huu. Tuna matumaini makubwa toka kwao kwa ajili ya kuboresha ufanisi wa TBC katika tasnia ya Utangazaji katika ulimwengu wa Teknolojia inayobadilika kwa kasi kubwa duniani.


Ni imani yangu kwamba Bodi hii mpya italeta msukumo mpya katika utendaji wa Shirika ili hata watumishi wanaofanya kazi katika shirika hili waendelee kujivunia kuwa ndani ya TBC lakini pia Umma wa Watanzania wajivunie viwango vya utendaji wa Shirika hili.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527