WANANCHI WATUMIA MABANGO KUFIKISHA UJUMBE KWA RAIS MAGUFULI




Wakati muda wa `mapumziko’ ya bomoabomoa ukimalizika leo huku jaribio la kupata zuio la muda likiwa limewekwa kiporo, wakazi wa Jangwani ambako nyumba zitaanza kubomolewa leo, jana waliweka mabango barabarani yanayotuma ujumbe wa aina mbalimbali kwa Rais John Magufuli.

Bomoabomoa hiyo ilianza Desemba mwaka jana likilenga nyumba zilizojengwa kwenye Bonde la Mto Msimbazi, lakini lilisitishwa kwa siku 14 na Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, William Lukuvi hadi Januari 5, mwaka huu kuwapa nafasi wakazi kuondoka kwa hiari yao kuokoa mali zao.


Wakazi wa Jangwani walitumia mwanya huo wa kusitisha ubomoaji, kufungua kesi Mahakama ya Ardhi kupinga kuondolewa maeneo hayo bila ya kupatiwa sehemu nyingine na kuwasilisha ombi za zuio la ubomoaji, lakini chombo hicho cha sheria kilikataa kubariki mambo hayo ya kutaka sitisho la bomoabomoa liendelee wakati kesi ikiendelea mahakamani.


Wakati wawakilishi wa wakazi hao wakiwa mahakamani katikati ya jiji, watumishi wa halmashauri za jiji waliendelea kuweka alama nyumba zinazotakiwa kubomolewa wakiwa wamesindikizwa na ulinzi mkali wa polisi.


Hakukuwepo na wakazi waliojitokeza kuzuia uwekaji alama hiyo ya “X” inayotaarifu kuwapo kwa ubomoaji, lakini mabango ya maboksi yaliyosimikwa kwenye vifusi na maeneo mengine ya jangwani, yanatosha kuelezea hisia za wakazi hao wanaoishi maeneo ambayo yametangazwa kuwa hatarishi.





Chanzo-Mpekuzi blog

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527