KUHUSU WATU WATATU WANAODAIWA KUUA WATU WANNE KWA KUWAKATA MAPANGA KISHA KUWAFUNIKA MAJANI YA MIGOMBA BARABARANI HUKO KAGERA




Jeshi la Polisi mkoani Kagera linawashikilia watu watatu wanaotuhumiwa kuhusika na mauaji ya kikatili ya watu wanne waliokuwa wakazi wa kijiji cha Ilogelo kilichoko katika kata ya Katoma kwa kuwakata kata na mapanga na kisha kutelekeza miili ya marehemu hao kandoni mwa barabara huku wakiwa wamefunikwa na majani ya migomba. 


Akizungumza na waandishi wa habari ofisi kwake kamanda wa jeshi la Polisi mkoani Kagera, Augustine Ullomi ambaye ni kamishina msaidizi mwandamizi amesema kuwa watu hao wametiwa mbaroni kufuatia upelelezi wa kina uliofanywa na jeshi hilo kwa kushirikiana na wananchi na kuongeza kuwa jeshi hilo linaendelea na kufanya upelelezi zaidi juu ya tukio hilo la mauaji ya kikatili na watakaothibitika watafikishwa mahakamani. 


Aidha, kamanda Ullomi amesema matukio ya mauaji katika mkoa wa Kagera kuwa kamwe hayatavumiliwa kwa kuwa yanahatarisha amani na usalama hivyo amewaomba wananchi waendelee kutoa ushirikianoi kwa jeshi hilo ili liweze kuwabaini na hatimaye kuwashughulikia wale wote wanaojihusisha na vitendo vya uharifu. 


Akizungumza juu ya tukio jingine amesema watu wenye hasira wamemuua jambazi mmoja aliyekuwa miongoni mwa majambazi wanne waliomvamia Dominic Lwabushaka mkazi wa kijiji cha Bunyinya kilichoko wilayani Karagwe na kumpora jumla ya shilingi milioni mbili, amemtaja jambazi aliyeuwawa kwa jina la Juma Byarugaba, amesema majambazi wengine waliokuwa na marungu na mapanga walifanikiwa kuwaporonyoka wananchi.
  Via>>ITV

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post