KUHUSU ASKARI WANNE NA RAIA WATATU KUUAWA KWA KUPIGWA RISASI NA MAJAMBAZI KWENYE KITUO CHA POLISI TANZANIA







Watu saba wameuawa kwa kupigwa risasi miongoni mwao askari polisi wanne, mtuhumiwa mmoja pamoja na raia wawili ambapo askari mmoja amejeruhiwa huku watoto wanaokadiriwa kuwa na umri wa miaka minne hadi mitano wakinusurika kifo katika kituo cha polisi cha Sitaki Shari baada ya watu wanaodhaniwa kuwa ni majambazi kuvamia kituo hicho na kuiba silaha ambazo idadi yake kamili haijafahamika.


Tukio hilo linalotajwa kuwa ni la kuogofya limetokea jijini Dar es Salaam katika kituo hicho ambapo Mwandishi wa habari hizi ameshuhudia madimbwi ya damu,maganda ya risasi pamoja na visu ambapo mashuhuda wamesemea kuwa mmoja wa mtuhumiwa aliyeuawa amepigwa risasi na majambazi wenzie baada ya pikipiki aliyokuwa akiitumia kushindwa kuwaka ili kuondoka katika eneo la tukio baada ya kutekeleza uhalifu huo ambapo watoto watatu waliofahamika kwa majina ya lea, Recho na Richard waliokuwa wamehifadhiwa katika kituo hicho baada ya kupotea wakinusurika.

Katika eneo la tukio ambalo ulinzi ulikuwa umeimarishwa vikali na askari polisi waliokuwa na silaha nzito pamoja na mabomu ya machozi wananchi walitakiwa kukaa mbali na tukio huku wakiwa wamejikusanya katika makundi kutafakari tukio hilo la aina yake ambapo baadhi yao wametoa ushauri kwa jeshi la polisi ili kukabiliana na uhalifu mpya wa kuvamia vituo vya jeshi la polisi.

Mwenyekiti wa kamati ya ulinzi na usalama ambaye pia ni mkuu wa mkoa wa Dar es Salaam Mh Said Meck Sadiq ameelezea tukio hilo kuwa ni la aina yake na kutaka ushirikiano kutoka kwa wananchi kuwezesha kuwakamata wahalifu hao huku akiongeza kuwa nyakati za kuaminiana zimeanza kutoweka na hivyo ni vyema kuwatilia mashaka hatawale wanaoonekana kwenda katika nyumba za ibada kwa kuwa mipango ya uhalifu baadhi yake husukwa na kupangwa kwenye nyumba hizo za ibada.

Mkuu wa jeshi la polisi Ernest Mangu ni miongoni mwa viongozi wa ngazi za juu wa jeshi hilo aliyefika katika eneo la tukio na mara baada ya kukagua na kupata maelezo ya tukio hilo ameonesha kusikitishwa na kutamka kulaani kwa nguvu zote tukio hilo huku akiongeza kuwa tukio hilo lina viashiria vya kigaidi huku akishindwa kutaja idadi ya silaha zilizoibwa kwa madai ya sababu za kiitelijensia na uchunguzi utakapokamilika taarifa rasmi itatolewa lakini akakiri kuchukuliwa kwa baadhi ya silaha.
Via>>Itv

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post