Buriani Jean Marie Ntagwabila |
KOCHA Jean Marie Ntagwabila aliyekuwa atue Simba SC Januari mwaka huu
kuwa Msaidizi wa Mserbia, Goran Kopunovic katika klabu ya Simba SC
amefariki dunia leo nchini Rwanda.
Ntagwabila amefariki ghafla katika hospitali ya Jeshi, Kanombe baada ya kusumbuliwa na ugonjwa wa mapafu.
Simba SC ilikuwa kwenye mchakato wa kumleta marehemu afanye kazi na
Goran, lakini Mserbia huyo alimkataa na akapendekeza aletwe Mnyarwanda
mwingine, Alphonse Gatera aliyekuwa Msaidizi wake wakati anafundisha
Polisi ya Rwanda.
Marehemu atakumbukwa nchini Rwanda kwa kazi nzuri aliyoifanya wakati wa
uhai wake, ikiwemo kuifanya APR iwe tishio mno kiasi cha kufikia
kuifunga Zamalek ya Misri mabao 4-1 mwaka 2004 katika Raundi ya Kwanza
ya Ligi ya Mabingwa Afrika, ikitoka kufungwa 3-2 katika mchezo wa
kwanza Cairo.
APR ilisonga mbele hatua ya 16 Bora, ambako ilikwenda kutolewa kwa
mbinde na Africa Sports ya Ivory Coast kwa penalti baada ya sare ya
jumla ya 1-1, kila timu ikishinda 1-0 nyumbani kwake. Bwana ametoa,
bwana ametwaa. Pumzika kwa amani Jean Marie Ntagwabila.
Chanzo- kengete.com