Mwanamme
asiyefahamika jina wala makazi yake ameuawa kwa kunyongwa shingo kisha mwili
wake kutundikwa juu ya mti kwa kutumia suruali aliyokuwa amevaa na watu
wasiofahamika katika kijiji na kata ya Ibadakuli manispaa ya Shinyanga mkoani
Shinyanga.
Kaimu
kamanda wa polisi mkoa wa Shinyanga SSP Longinus Tibishubwamu alisema tukio
hilo limetokea Januari 27,mwaka huu saa 10:46 jioni katika kijiji cha Ibadakuli
ambapo mwanamme (30-35) huyo asiyejulikana jina,kabila wala makazi yake aliuawa
kisha mwili wake kutundikwa juu ya mti.
Kamanda
Tibishubwamu alisema mwanamme huyo aliuawa na watu wasiofahamika kisha
mwili wake kutundikwa juu ya mti kwa kutumia suruali aliyokuwa amevaa.
Alisema
mwili wa marehemu umekutwa na jeraha kwenye kidole cha mguu wa kulia na
uchunguzi wa daktari unaonyesha kuwa marehemu alinyongwa shingo na chanzo cha
mauaji hayo bado hakijajulikana.
Wakati huo
huo mwanamke asiyefahamika jina wala makazi yake anayekadiriwa kuwa na umri
kati ya 25 na 30 ameuawa kisha mwili wake kuwekwa chini ya daraja dogo lililopo
katika kitongoji cha Jihingu kata ya Kolandoto manispaa ya Shinyanga.
Kamanda
Tibishubwamu alisema tukio hilo limetokea Januari 27,mwaka huu saa 12:00
jioni katika kitongoji cha Jihingu ambapo mwanamke huyo aliuawa na watu wasiofahamika
kisha mwili wake kuwekwa chini ya daraja dogo lililopo katika kitongoji hicho.
Aliongeza
kuwa mwili wa marehemu umekutwa ukiwa na majeraha kichwani,usoni na ubavu wa
kulia na kwamba jeshi la polisi linafanya uchunguzi juu ya mauaji hayo ili kuwabaini
na kuwakamata wahusika.
Na Kadama Malunde-Shinyanga