MADIWANI WA SHINYANGA WAPEWA MAKAVU LIVEEE!!!

 
Naibu meya wa manispaa ya Shinyanga ndugu David Nkulila-picha na Kadama Malunde-Malunde1 blog
Madiwani katika manispaa ya Shinyanga wametakiwa kutimiza wajibu wao kwa kusimamia ipasavyo miradi mbalimbali ya maendeleo badala ya kuogopa kupoteza nyadhifa zao katika chaguzi zijazo endapo watasimamia kikamilifu kuhimiza wananchi kutoa michango.

Akizungumza juzi katika kikao cha Baraza la madiwani wa manispaa ya Shinyanga mwenyekiti wa kikao hicho ambaye ni naibu meya wa manispaa hiyo David Nkulila alisema kuna baadhi ya madiwani hivi sasa hawawajibiki wakihofia kunyimwa kura katika chaguzi zijazo.

Nkulila alisema wapo madiwani ambao wanashindwa kuwahamasisha wananchi kuchangia miradi ya maendeleo kama vile ujenzi wa maabara katika shule kwa kile kinachodaiwa kuogopa kuwachosha kwa michango wapiga kura wao.

“Najua wengi wetu tuna hofu kubwa na chaguzi zijazo,naomba muwe  wajasiri kuelimisha wananchi kwa kusema yaliyo kweli,simamieni miradi ya maendeleo,kama ni kurudi kwenye nafasi zenu mungu ndiyo anajua,tendeni haki kwa wananchi,uoga haufai”,aliongeza Nkulila.

Akitangaza maeneo mapya ya uchaguzi wa serikali za mitaa mwaka huu,mkurugenzi wa manispaa ya Shinyanga  Festo Kang'ombe alisema tayari kanuni za uchaguzi huo zimeshatoka na kilichobaki ni kupokea vifaa kwa ajili ya kupigia kura tarehe 14,Desemba mwaka huu.

Kang’ombe alisema uchaguzi utafanyika katika kata 17 ikihusishwa mitaa 55 badala ya 25 ya chaguzi zilizopita,vijiji 19 badala ya 17 na vitongoji 85.

“Tayari tumeshatoa tangazo kuhusu  maeneo mapya ya uchaguzi wa serikali za mitaa,matangazo yapo katika ofisi za kata na manispaa ya Shinyanga”,alisema Kang'ombe

Kwa upande wake diwani wa kata ya Ndala kupitia Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) George Sungura alieleza kusikitishwa na madiwani katika manispaa hiyo kukosa ushirikiano wa dhati katika shughuli za maendeleo huku akiwataka kubadilika ili kuwaletea maendeleo wananchi.
 Na Kadama Malunde-Shinyanga

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post