Baadhi ya wakazi wa Kitongoji cha Kashalami Kata ya Mashimboni wilaya ya Mlele Mkoa wa Katavi wamelazimika kushinda juu ya miti kwa kuhofia kushambuliwa na Kiboko aliyevamia kijiji hicho na kuhatarisha uhai wa Wanachi
Kwa mujibu wa Diwani wa Kata hiyo ya Mashimboni Raphael Kalinga tukio hilo lilitokea hapo Agosti 18 majira ya saa moja na nusu asubuhi
Akielezea tukio hilo alisema Kiboko huyo baada ya kuvamia kijiji hicho alielekea kwenye nyumba ya mkazi mmoja aitwaye Joseph Kashamakula ambaye alinusurika kushambuliwa na kiboko huyo wakati alipokuwa akitokea chooni kujisaidia
Diwani Kalinga alisema ndipo Kiboko huyo ambae alionekana kuwa na hasira alipoanza kukanyaga kanyanga na kuvivunja vyombo vya mwanakijiji huyo ambavyo vilikuwa nje ya nyumba yake na kuviharibu kabisa hali ambayo ilimfanya mwananchi huyo apige mayowe ya kuomba msaada kwa majirani
Majirani walifika kwenye eneo hilo hata hivyo walilazimika kutimua mbio baada ya kiboko huyo kuanza kuwafuata hali ambayo ilipelekea kukimbia na kisha kupanda juu ya miti kwa kuhofia kushambuliwa na mnyama huyo ambaye aliendelea kuvunja vyombo kwenye nyumba mbalimbali
Alisema Kiboko huyo aliendelea kuzunguka kwenye eneo la kijiji hicho na taarifa za zilifika kwenye Idara ya Maliasili ya Halmashauri ya Nsimbo ambao walituma Akari wao wa wanyama pori kwenda huko
Baada ya Askari wa Maliasli kufika kijijini hapo walianza msako wa kumtafuta kwa kushirikiana na wananchi ambapo walifanikiwa kumwona na kisha walimuua kwa kumpiga Risasi tumboni na kichwani
Diwani Kalinga alieleza baada ya Kiboko kuuwa wananchi licha ya hapo awali kumkimbia kiboko huyo walianza kugombea nyama ya mnyama huyo kwa kuchukua kitoweo cha mboga na baada ya nusu saa wakawa wamemmaliza.
Na Walter Mguluchuma-Mpanda Katavi