ANGALIA PICHA KIGOGO AMCHOMA KISU MKEWE NA KUMTOA MANUNDU



Sehemu ya mguu alipochomwa kisu na Bw. Mugaka (mumewe).

KIGOGO wa shirika moja la kimataifa linalojishughulisha na watoto yatima, tawi la mkoani Pwani, Tanzania aliyetajwa kwa jina moja la Mugaka, anayekadiriwa kuwa na umri kati ya miaka 35 hadi 40, ametupwa rumande akituhumiwa kumchoma kisu na kumtoa manundu mkewe, Leah (28).

Tukio hilo la kusikitisha lilijiri wilayani Kisarawe, Pwani mwishoni mwa wiki iliyopita. Kwa mujibu wa habari zilizopatikana, chanzo cha unyama huo kinashangaza huku madai ya Mugaka ambaye ni afisa mshauri wa shirika hilo yakisema mkewe huyo amekuwa akimjazia choo kwa kuwa tangu amuoe miaka mitatu iliyopita, ameshindwa kumzalia mtoto.

 Habari ziliendelea kudai kwamba shirika analofanyia kazi Mugaka linalosimamiwa na mfuko wa rais wa zamani wa Marekani, Bill Clinton.

 Madai mazito yalishushwa kwamba Mugaka amekuwa akimnyanyasa mkewe kwa sababu hiyo, kiasi cha kumtolea maneno ya kejeli, dharau, kashfa huku akimshushia kipigo ‘hevi’.

Majeraha mengine sehemu ya mguu wa kulia.
 Ilisemekana kwamba ilifika wakati hali ikawa mbaya kiasi cha baadhi ya majirani kumshauri Mugaka kuachana naye kama anaona hamfai. Ilisemekana kwamba chanzo cha kufanyiwa unyama huo na kujeruhiwa na kisu ni madai ya mwanaume huyo kuwa alitumiwa ujumbe mfupi kwenye simu yake, akiambiwa kuwa mkewe alikuwa akimsaliti kwa kutembea na watu wa nje, wakiwemo polisi. 

Kigogo anayetajwa kwa jina moja la Mugaka anayetuhumiwa kumnyanyasa mkewe.
 Ilidaiwa kwamba mkewe alikataa madai hayo na kumtaka mumewe kuitoa namba ya simu iliyotuma ujumbe huo ili wampigie palepale wakiwa wote, lakini jamaa huyo alikataa na kumshambulia sehemu mbalimbali za mwili huku akimchoma na kisu pajani. 

Jirani wa mtuhumiwa aliyeomba hifadhi ya jina alidai kwamba Mugaka amekuwa akimpiga, kumtesa, kumdhalilisha mkewe mara kwa mara huku akisikika kumweleza kuwa ipo siku atamuua.

Muonekano wa karibu wa Bi. Leah.

 Baba mzazi wa majeruhi, William Lyima alisema baada ya kupata taarifa za kipigo hicho, alimpigia simu Mkuu wa Kituo cha Polisi cha Kisarawe, OCD Issa na kumtaarifu tukio hilo ambapo askari wake walifika na kuizingira nyumba ya mtuhumiwa huyo na ilipofika majira ya saa 11:00 alfajiri walifanikiwa kumtia mbaroni.

Kigogo huyo amefunguliwa mashitaka ya shambulio la kudhuru mwili na kujeruhi kwa kisu katika jalada lenye kumbukumbu namba KIS/RB/964/2014-SHAMBULIO LA KUDHURU NA KUJERUHI MWILI akisubiri sheria kuchukua mkondo wake.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527