WATU WATATU WAFARIKI DUNIA BAADA YA KULA FUTARI YENYE SUMU HUKO TANGA


Watu watatu wa familia moja, wakazi wa Kijiji cha Kwasunga wilayani Handeni mkoani Tabora wamekufa baada ya kula futari ya mihogo inayosadikiwa kuwa na sumu.

Akizungumza na waandishi wa habari jana, kamanda wa polisi wa Mkoa wa Tanga, Constantine Massawe alisema tukio hilo lilitokea juzi saa 1:00 usiku eneo la Kwasunga Handeni na maiti zimehifadhiwa katika Hospitali ya Wilaya ya Handeni.

Kamanda Massawe aliwataja waliokufa kuwa ni Juma Jumbe (6), Abdi Jumbe (10) na Ramadhani Jumbe (15). 

Pia alisema kuwa wazazi wa watoto waliwahishwa hospitali ambako walipatiwa matibabu na wanaendelea vizuri.
Kamanda Massawe alisema kwa mujibu wa wazazi wa watoto hao, walikula futari hiyo na baada ya kumaliza, walianza kujihisi vibaya sambamba na kuishiwa nguvu na alianza kuanguka mmoja baada ya mwingine.

“Chanzo cha kifo ni futari ya mihogo ambayo kwa mujibu wa vipimo ilikuwa na sumu. Wazazi wao wako hai ila nao walikuwa katika hali mbaya, lakini baada ya kupatiwa matibabu wanaendelea vizuri,” alisema kamanda huyo.

Kamanda huyo aliwataka wote walio katika mfungo kuichunguza mihogo wanayoinunua kwa ajili ya matumizi ya futari kwani baadhi haifai kuliwa na binadamu.

Mhogo unajulikana vyema,Kama mtu ukiumenya na kuona una rangi za ajabu ajabu ndani, basi achana nao usiupike mingine haifai kuliwa na binadamu,” alisema Massawe. 

Alitoa wito kwa watu kuwa makini. 

via>>mwananchi

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post