Maadhimisho Miaka 51 ya Tanzania Bara Yafana Jijini Dar es Salaam, JK Aongoza


Amiri Jeshi mkuu na Rais wa Jamhuri ya Muungano ya Tanzania,Dk. Jakaya Mrisho Kikwete akiwasili katika Uwanja wa Uhuru akiwa kwenye gari maalumu la Kijeshi sambamba na Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi na Usalama,Jenerali Davis Mwamunyange walipokuwa wakitoa salamu kwa wananchi na wageni mbalimbali waliofika uwanjani kwa ajili ya sherehe za maadhimisho ya Miaka 51 ya Uhuru wa Tanzania Bara (Tanganyika).

Na Joachim Mushi
RAIS
wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Kikwete leo ameongoza Sherehe za Maadhimisho ya Miaka 51 ya Uhuru wa Tanzania Bara (Tanganyika) yaliyofanyika kwenye Uwanja vya Uhuru jijini Dar es Salaam na kuhudhuriwa na viongozi na wageni mbalimbali kutoka nje na ndani ya nchi.

Rais Kikwete aliwasili katika uwanja huo majira ya saa nne kamili na kuwasalimu Watanzania na viongozi mbalimbali waliohudhuria sherehe hizo kabla ya kupigiwa mizinga 21 ikiwa ni heshima kama Amiri Jeshi Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi na Usalama wa nchi.

Baadaye Rais Kikwete alikagua gwaride rasmi la maadhimisho hayo kisha gwaride hilo lililoundwa na askari anuai kutoka majeshi ya ulinzi na usalama wa nchi. Gwaride pia lilipita mbele ya rais kutoa heshima kwa mwendo wa pole na haraka ambapo lilikuwa ni kivutio kingine kwa wageni waalikwa waliofika katika sherehe hizo.

Katika maadhimisho ya mwaka huu Rais Kikwete alilazimika kusimama na kuzungumza ikiwa ni tofauti na sherehe zilizopita za uhuru, ambapo alifanya hizo ikiwa ni kutoa shukrani kwa wageni mashughuli 12 kutoka nchi mbalimbali ambao wamehudhuria sherehe hizo.

Viongozi mbalimbali wakiwa katika maadhimisha hayo, kutoka kulia ni Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, Joseph Kabila, Mama Maria Nyerere, Rais wa Msumbiji, Armando Guebuza, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano ya Tanzania, Dk. Mohamed Gharib Bilal na Rais Mstaafu wa Awamu ya pili, Mzee Ali Hassan Mwinyi. (Picha zote na Full Shangwe Blog)

Miongoni mwa wageni hao wamo marais watatu, yaani Rais wa Msumbiji, Armando Guebuza, Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC), Joseph Kabila, pamoja na Rais wa Namibia, Hifikepunye Pohamba.

Wengine ni Makamu wa Rais wa Malawi, Khumbo Kachali, Makamu wa Rais Zambia, Dk. Guy Scott, Makamu wa Rais wa Angola, Manuel Vicente, Makamu wa Rais wa Visiwa vya Shelisheli, Waziri Mkuu wa Lesotho, Thomas Motsoahae Thabane, Waziri Mku wa Swatzland, Waziri Mkuu wa Rwanda, Waziri wa Mambo ya Nje ya Zimbabwe, Katibu Mkuu Mtendaji wa SADC na viongozi wengine kutoka nje na ndani ya nchi.

Sherehe hizo za mwaka huu zilizopambwa na vikundi vya halaiki, maonesho ya sura ya kitabu, vikundi vya ngoma na sarakasi yaliudhuriwa pia na viongozi wa juu wa Serikali ya Tanzania Bara na Visiwani, viongozi anuai wa vyama na Serikali pamoja na viongozi wa dini.

Katika mazungumzo yake mafupi kwa umma huo, aliwapongeza Watanzania kwa kutimiza miaka 51 ya Uhuru wa Tanzania Bara huku wakiendelea kudumisha amani na utulivu na mafanikio tele katika nyanja anuai. Kivutio kingine katika maadhimisho hayo ambacho kiliwainua viongozi mbalimbali kwenye viti ni ngoma ya kikundi cha Utandawazi kutoka Ukerewe ambayo ilichezwa kiumahiri na mvuto na watoto wadogo wenye umri wa miaka mitatu kitendo ambacho kiliwavutia wengi. Kauli mbiu ya Maadhimisho ya Mwaka huu ni “Uwajibikaji, Uadilifu na Uzalendo ni nguzo ya Maendeleo ya Taifa letu”.

                                           http://www.thehabari.com

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments