MGANGA MFAWIDHI HOSPITALI YA WILAYA LINDI AISHUKURU SERIKALI KWA UMEME WA REA

Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Wilaya ya Lindi, Dkt. Kassanga Benito (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Ujumbe kutoka REA waliotembelea hospitali hiyo wakiwa katika ziara ya kazi kukagua utekelezaji wa miradi ya nishati vijijini, Januari 27, 2023. Wa tatu kutoka kulia ni Mjumbe wa Bodi ya Nishati Vijijini (REB), Oswald Urassa ambaye aliongoza Ujumbe huo.

Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Wilaya ya Lindi, Dkt. Kassanga Benito (katikati) akiwa na Ujumbe kutoka REA waliotembelea hospitali hiyo wakiwa katika ziara ya kazi kukagua utekelezaji wa miradi ya nishati vijijini, Januari 27, 2023. Kulia kwake ni Mjumbe wa Bodi ya Nishati Vijijini (REB), Oswald Urassa ambaye aliongoza Ujumbe huo.

Mjumbe wa Bodi ya Nishati Vijijini (REB), Oswald Urassa na Ujumbe wake, wakikagua miundombinu ya umeme jirani na hospitali wa Wilaya ya Lindi, walipokuwa katika ziara ya kazi kukagua utekelezaji wa miradi ya nishati vijijini, Januari 27, 2023.


Baadhi ya majengo ya Hospitali ya Wilaya ya Lindi. Hospitali hii imenufaika na umeme wa REA. Taswira ilichukuliwa Januari 27, 2023 wakati wa ziara ya Ujumbe kutoka REA ukiongozwa na Mjumbe wa Bodi ya Nishati Vijijini (REB), Oswald Urassa kukagua utekelezaji wa miradi ya nishati vijijini.


Watumishi wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA), Omari Sengulo (kulia) na Mohamed Ismail wakiwa katika viunga vya Hospitali ya Wilaya ya Lindi wakati wa ziara ya viongozi wa REA kukagua utekelezaji wa miradi ya nishati vijijini mkoani Lindi, Januari 27, 2023. Hospitali hiyo imenufaika na Mradi wa Umeme Vijijini.

………………………………………..

Veronica Simba – Lindi

Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Wilaya ya Lindi, Dkt. Kassanga Benito, ameishukuru Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) kwa kubuni na kuendelea kutekeleza miradi ya umeme vijijini ambayo imewezesha uboreshaji wa huduma katika sekta mbalimbali, ikiwemo afya.

Aliyasema hayo Januari 27, 2023 wakati akizungumza na Ujumbe kutoka REA ulioongozwa na Mjumbe wa Bodi ya Nishati Vijijini (REB), Oswald Urassa, ukiwa katika ziara ya kazi kukagua utekelezaji wa miradi ya nishati vijijini.

Akieleza furaha yake, Dkt. Benito alisema Hospitali hiyo ya Wilaya ya Lindi ni miongoni mwa wanufaika wa umeme vijijini na kwamba nishati hiyo imewezesha utoaji huduma zote muhimu za afya kwa wananchi kwa ufanisi jambo ambalo lisingewezekana pasipo kuwa na umeme.

“Tunatoa huduma karibu zote kubwa za afya na kwa sasa tumeanzisha kambi ya upasuaji hospitalini hapa huku tukijipanga kuendelea kuongeza huduma nyingine mbalimbali,” amefafanua Mganga Mfawidhi.

Aidha, alitaja manufaa mengine ya uwepo wa umeme hospitalini hapo kuwa ni pamoja na kuwezesha kuhifadhi damu huduma ambayo isingewezekana pasipo umeme.

Kwa upande wake, Mjumbe wa Bodi alimhakikishia Dkt. Benito kuwa Bodi ya Nishati Vijijini itaendelea kuisimamia REA ipasavyo ili kuhakikisha miradi ya nishati vijijini inaendelea kutekelezwa kwa tija nchini kote kwa manufaa ya wananchi na Taifa kwa ujumla.

Hospitali ya Wilaya ya Lindi ilianza kutoa huduma za afya kwa wananchi mwaka 2020. Kabla ya hapo, wnanchi walikuwa wakipata huduma hizo katika hospitali ya Nyangao.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments