DC MBONEKO : TUMIENI FEDHA ZA TASAF KUJIKWAMUA KIUCHUMI


Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Jasinta Mboneko akizungumza na walengwa wa TASAF wa vijiji vya Mwashagi na Kimandaguli Kata ya Lyabukande wilayani Shinyanga.

Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Jasinta Mboneko akiendelea kuzungumza na walengwa wa TASAF.

Walengwa wa TASAF wakisikiliza Nasaha za Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Jasinta Mboneko.

Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Jasinta Mboneko na Diwani wa Lyabukande Luhende Kawiza, wakipiga picha ya pamoja na walengwa wa TASAF.

Na Marco Maduhu, Shinyanga

MKUU wa wilaya ya Shinyanga Jasinta Mboneko, amewataka walengwa wa Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF), wenye mpango wa Kunusuru Kaya Maskini, wazitumie fedha hizo kujikwamua kiuchumi pamoja na kupeleka watoto shule.

Mboneko alibainisha hayo jana wakati akizungumza na walengwa wa TASAF wa Vijiji vya Mwashagi na Kimandaguli Kata ya Lyabukande wilayani Shinyanga katika Ofisi ya Mtendaji Kimandaguli, wakati walengwa hao walipokuwa wakijaza fomu na kusabili kupokea fedha zao.

Amesema anataka kuona fedha hizo za TASAF walengwa wanazitumia vizuri kujiletea maendeleo na kuinuka kiuchumi, ikiwamo kufuga mifugo ili waondokane na umaskini kabisa, sababu baadhi ya walengwa fedha hizo zimeshabadili mfumo wa maisha yao ikiwamo kujenga nyumba imara.

“Nataka nione maendeleo kwenye fedha hizi za TASAF mzitumie vizuri kujikwamua kiuchumi pamoja na kupeleka watoto shule,”amesema Mboneko.

“Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan, ameleta fedha hizi ili ziwakwamue kiuchumi hivyo ni vyema mkazitumia vizuri na kubadili maisha yenu, na pia mkituma wawakilishi kuja kuwachukulia hela tumeni wale waaminifu ili wasizidokoe,”ameongeza.

Nao baadhi ya walengwa hao wa TASAF wameishukuru Serikali kwa kuwapatia fedha hizo ambazo zimekuwa mkombozi wa maisha yao, na kuahidi kuzitumia vizuri na kutoka kwenye dimbwi la umaskini.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments