DC MBONEKO, MD SATURA, MEYA MASUMBUKO & MAKUNE WANG'OA TUZO ZA UONGOZI BORA


Na Kadama Malunde - Malunde 1 blog
Baraza la Madiwani Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga limewapatia Tuzo za Uongozi Bora kwa mwaka 2021/2022 Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga Jasinta Mboneko, Mstahiki Meya wa Manispaa ya Shinyanga Elias Ramadhani Masumbuko na Naibu Meya wa Manispaa ya Shinyanga Ester Festo Makune huku Mkurugenzi wa Manispaa hiyo, Jomaary Mrisho Satura akipatiwa Tuzo ya Utendaji Bora, Usimamizi wa RasilimaliWatu, Miradi na Mapato kwa Mwaka 2021/2022.


Tuzo hizo zimetolewa leo Jumatatu Agosti 22,2022 wakati wa Kikao cha Baraza la Madiwani wa Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga kilichofanyika katika ukumbi wa ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga.

Akitangaza Tuzo hizo, Mnadhimu wa Madiwani wa Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga, Hassan Mwendapole ambaye ni Mjumbe wa Kamati ya Fedha ya Halmashauri hiyo na Diwani wa Kata ya Kambarage amesema wameamua kutoa tuzo hizo ili kutoa hamasa (Motisha) na kutambua mchango mkubwa wa viongozi kwenye Halmashauri hiyo kwa mwaka 2021/2022.

“Mwaka huu tumeamua tujipongeze sisi wenyewe ili kuongeza nguvu ya kuleta maendeleo katika Manispaa yetu. Tunawapatia Tuzo za Uongozi Bora kutokana na umahiri na uchapakazi wao lakini pia kila mmoja wao atapatiwa shilingi 500,000/=.

Tumetoa tuzo hizi kufuatia Manispaa ya Shinyanga kushika nafasi ya kwanza katika Manispaa zote nchini katika ukusanyaji wa mapato kwa asilimia 126 tuzo zilizotolewa na Waziri wa TAMISEMI, Innocent Bashungwa lakini pia Manispaa yetu imekuwa ya kwanza nchini katika kundi la Manispaa zote na kupata tuzo ya utendaji bora katika usimamizi wa Rasilimaliwatu na utawala bora ambapo tuzo hiyo iliyolewa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Jenista Mhagama”,amesema Mwendapole.


“Mhe. Mkuu wa wilaya Jasinta Mboneko tangu afike katika wilaya ya Shinyanga amekuwa msaada mkubwa kwenye halmashauri hii,Huyu Mkurugenzi wetu tangu afike katika Halmashauri hii ameonesha juhudi kubwa katika kuibadilisha halmashauri, tunampa tuzo ya uongozi bora, usimamizi wa miradi na mapato ya Manispaa, anabana matumizi yasiyo ya lazima. Sambamba na hayo Mstahiki Meya Elias Ramadhani Masumbuko na Naibu Meya Ester Festo Makune tunawapatia tuzo ya Uongozi bora kwa mwaka 2021/2022”,amesema Mwendapole.

Akikabidhi Tuzo hizo, Katibu Tawala Mkoa wa Shinyanga Prof. Sizza Donald Tumbo amepongeza Madiwani wa Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga, Mkuu wa Wilaya, Mkurugenzi, Meya na watumishi wa Manispaa hiyo kwa ushirikiano na maelewano waliyonayo hali inayoongeza chachu ya maendeleo.

“Kwenye Halmashauri ambayo kuna maelewano lazima maendeleo yawepo,katika baadhi ya maeneo niliyopita ni nadra sana kukuta Mkurugenzi wa Halmashauri anaelewana na Madiwani au Meya kuelewana na Madiwani, Mkuu wa wilaya kuelewana Mkurugenzi, Mkuu wa wilaya na Meya au DC na Madiwani….Hongereni sana Manispaa ya Shinyanga kwa Maelewano yenu”,amesema Prof. Tumbo.

“Mahali ambapo upendo upo, maendeleo yapo. Endelezeni maelewano kwani sehemu ambayo haina maelewano hakuna maendeleo. Endeleeni na tunu hii ya upendo. Lakini pia toeni pia motisha kwa wafanyakazi boraa ngazi za chini ili kuwapa hamasa ya kufanya kazi vizuri”,amesema Prof. Tumbo.

Naye Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga, Jasinta Mboneko amewashukuru Madiwani wa Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga kwa kuandaa tuzo hizo kupitia kamati ya Fedha huku akiahidi kuwa yeye na wenzake waliopata tuzo hizo wataendelea kufanya kazi kwa uaminifu na uadilifu mkubwa.

“Kwa kweli mmetu - Supprise sana (Mmetushtukiza) hakujua kama mmetuandalia tuzo, tutaendelea kuwa watumishi waaminifu na waadilifu na kasi (Speed) itaongezeka zaidi. Tuendelee na mshikamano na upendo huu wa dhati mambo yaende vizuri. Mimi nipo tayari muda wote kufanya kazi za wananchi…na katika Wilaya yetu tumekuwa tukitoa hamasa kwa watumishi ngazi za chini kwa kuwapatia motisha mbalimbali”,amesema Mboneko.

Kwa upande wake, Mstahiki Meya wa Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga, Elias Ramadhani Masumbuko amewapongeza watumishi/watendaji wa Halmashauri hiyo kwa namna wanavyojituma kufanya kazi kwa bidii huku akimshukuru Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Jasinta Mboneko kwa namna anavyojitoa na kutoa mchango mkubwa kwa mambo mbalimbali ya maendeleo katika halmashauri hiyo.
Mnadhimu wa Madiwani wa Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga, Hassan Mwendapole ambaye ni Mjumbe wa Kamati ya Fedha ya Halmashauri hiyo na Diwani wa Kata ya Kambarage akitoa maelezo kuhusu Tuzo za Uongozi Bora zilizotolewa na Baraza la Madiwani wa Manispaa ya Shinyanga kwa Mkurugenzi wa Manispaa hiyo, Jomaary Satura, Meya wa Manispaa ya Shinyanga, Elias Ramadhani Masumbuko, Naibu Meya, Ester Makune na Mkuu wa wilaya ya Shinyanga, Jasinta Mboneko. Picha na Kadama Malunde - Malunde 1 blog
Katibu Tawala Mkoa wa Shinyanga Prof. Sizza Donald Tumbo (kushoto) akimkabidhi Tuzo ya Uongozi Bora kwa mwaka 2021/2022 Mstahiki Meya wa Manispaa ya Shinyanga, Elias Ramadhani Masumbuko.
Katibu Tawala Mkoa wa Shinyanga Prof. Sizza Donald Tumbo (kushoto) akimkabidhi Tuzo ya Uongozi Bora kwa mwaka 2021/2022 Naibu Meya wa Manispaa ya Shinyanga, Ester Festo Makune.
Katibu Tawala Mkoa wa Shinyanga Prof. Sizza Donald Tumbo (kushoto) akimkabidhi Tuzo ya Uongozi Bora kwa mwaka 2021/2022 Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga, Jasinta Mboneko.
Katibu Tawala Mkoa wa Shinyanga Prof. Sizza Donald Tumbo (kushoto) akimkabidhi Mkurugenzi wa Manispaa ya Shinyanga , Jomaary Mrisho Satura akipatiwa Tuzo ya Utendaji Bora, Usimamizi wa RasilimaliWatu, Miradi na Mapato kwa Mwaka 2021/2022.
Katibu Tawala Mkoa wa Shinyanga Prof. Sizza Donald Tumbo akizungumza wakati wa kukabidhi tuzo hizo.
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga, Jasinta Mboneko akizungumza baada ya kupokea Tuzo ya Uongozi Bora kwa mwaka 2021/2022.
Mstahiki Meya wa Manispaa ya Shinyanga, Elias Ramadhani Masumbuko akizungumza kwenye kikao cha Baraza la Madiwani wa Manispaa ya Shinyanga
Mkurugenzi wa Manispaa ya Shinyanga , Jomaary Mrisho Satura akizungumza kwenye kikao cha Baraza la Madiwani wa Manispaa ya Shinyanga.
Katibu Tawala Mkoa wa Shinyanga Prof. Sizza Donald Tumbo akipiga picha na viongozi waliopata tuzo pamoja na Madiwani wa Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga
Katibu Tawala Mkoa wa Shinyanga Prof. Sizza Donald Tumbo akipiga picha na viongozi waliopata tuzo pamoja na wajumbe wa kamati ya ulinzi na usalama wilaya ya Shinyanga.
Katibu Tawala Mkoa wa Shinyanga Prof. Sizza Donald Tumbo akipiga picha na viongozi waliopata tuzo pamoja na Watendaji/watumishi Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga
Katibu Tawala Mkoa wa Shinyanga Prof. Sizza Donald Tumbo akipiga picha na viongozi waliopata tuzo pamoja na wadau mbalimbali waliohudhuria kikao cha baraza la madiwani.

Picha zote na Kadama Malunde - Malunde 1 blog

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments