RC MTAKA AAGIZA WAZAZI WASIOPELEKA WATOTO SHULE WAPEWE ADHABU YA KUSAFISHA VYOO VYA SHULE

Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Anthony Mtaka akivuka daraja la mto Buluku  lililotengenezwa kwa muda baada ya kuharibiwa na mvua za masika zinazoendelea Wilayani Kondoa na kusababisha wanafunzi kushindwa kuhudhuria masomo.


*******
Na Dotto Kwilasa-Malunde 1 blog-KONDOA

MKUU wa Mkoa wa Dodoma,Anthony Mtaka amemwagiza Mkuu wa Wilaya ya Kondoa,Dk.Hamis Mkanachi kuwakamata   wazazi ambao watashindwa kuwapeleka wanafunzi shule kujiunga  kidato cha kwanza na kwamba mara baada ya kuwakamata wazazi hao  wanatakiwa kwenda kufanya usafi kwenye vyoo vya shule ili kuwaaibisha.

Mtaka amesema hayo mwishoni mwa wiki katika kijiji cha Bukulu Kata ya Bukulu Wilayani Kondoa na wanafunzi wa shule ya Sekondari Bukulu,Mkuu huyo wa Mkoa amemwagiza DC Mkanachi kuwakamata wazazi ambao watashindwa kuwapeleka shuleni watoto wao.

Licha hayo amewaagiza  Wakuu wa shule katika Wilaya hiyo kuanzisha Klabu za taaluma ili kuwasaidia wanafunzi waweze kufanya vizuri katika mitihani yao.

“Mwanafunzi asipofika Jumatatu (31 Januari) chukua mgambo  kamata wote waje wafanye usafi, waje wasafishe vyoo wapelekeni pale shuleni ili watoto wao wawe wanawaona, Wazazi wao wanavyodhalilika kwa sababu yao”amesema.

“Anzisheni Klabu za taaluma za Sayansi,Arts,Mazingira na Takukuru anzisheni midahalo ya form one na form two na form three na four  ili wanafunzi waweze kupata ulewa pamoja na kujifunza.Wapeni mitihani ya mara kwa mara Mkuu wa Wilaya una PHD lakini hali ya elimu hapa sio nzuri,”amesema.

Kwa upande wake,Mkuu wa Wilaya hiyo,Dk.Mkanachi  amewataka wanafunzi wa shule hiyo  kusoma kwa bidii kwani Serikali imeishawapelekea miundombinu ikiwemo ujenzi wa madarasa na walimu.

Naye,Mwenyekiti wa CCM Wilaya ya Kondoa,Mohammed Kova amesema kiujumla hali ya elimu Wilayani humo sio nzuri hivyo zinahitajika jitihada za pamoja ili kunusuru hali ya elimu.

“Nawaomba sana wanangu someni,someni mimi niliuza nyumba yangu Kondoa  ili nisomeshe watoto wangu sasa hivi wote wana kazi nzuri na mimi nakula matunda yao,tusomeshe,”amesema.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments