KAMPENI YA USAFI WA MAZINGIRA YAZINDULIWA SINGIDA...RC MAHENGE APIGA MARUFUKU NG'OMBE KUINGIZW KWENYE MAZIWA


Mkuu wa Mkoa wa Singida Dkt. Binilith Mahenge  akiongea wakati wa uzinduzi wa kampeni ya usafi wa mazingira.
Mkurugenzi wa  Halmashauri ya Manispaa ya Singida  Zefrin  Lubuva akizungumza
Mstahiki Meya wa Manispaa ya Singida  Yagi Kiaratu  (katikati) akiongea na wananchi katika uzinduzi wa kampeni ya usafi wa mazingira .
Wananchi waliojitokeza siku ya uzinduzi wa kampeni ya usafi wa mazingira .

Na Edina Malekela, Singida.

Ni siku kumi na mbili tangu Mkuu wa Mkoa wa Singida Dkt. Binilith Mahenge  kutoa agizo kwa Mkurugenzi wa Manispaa ya Singida  kufanyika usafi kwenye fukwe za maziwa ya Singidani na Munangi wakati wa ziara yake ya kikazi aliyoifanya mwanzoni mwa mwezi huu,leo amezindua kampeni hiyo ya usafi wa mazingira.

Kupitia agizo hilo la Mkuu wa Mkoa  sasa  Halmashauri ya Manispaa ya Singida imezindua kampeni ya usafi wa mazingira ambapo kwa sasa usafi kwa Mkoa utafanyika  kila Juma mosi.

Awali akisoma Taarifa Mkuu wa Idara ya mazingira  Halmashauri ya Manispaa  Arafa  Mohamedi amesema  lengo la kuzindua  kampeni ya usafi  wa mazingira ni kukumbushana na kuelimisha  kuhusu wajibu  wa kuhifadhi na kutunza mazingira kwa manufaa ya vizazi vya sasa na vijavyo.

Aidha  Arafa  amesema   suala la  uzururishaji  ovyo wa mifugo katikati ya mji ni tatizo lingine linalosababisha uharibifu na uchafuzi  wa  mazingira ongezeko la watu na utiririshaji  wa  maji machafu katika  mitaro na mifereji  wakati wa mvua.

Alisema zipo jitihada  zinazofanywa na Halmashaurj ya Manispaa ya Singida  katika kukabiliana na changamoto za uchafuzi wa mazingira lakini kikubwa ni kuendeleza  juhudi  zilizoanzwa za kampeni ya usafi wa mazingira.
 
Naye Mstahiki Meya wa  Halmashauri  ya Manispaa ya Singida Yagi Kiaratu  alisema kuwa wao kama Halmashauri  watahuisha timu zote ili kuweka  ulinzi wa Maziwa yasiendelee kuharibiwa na kuvamiwa na wananchi kwani maziwa hayo  ni fahari ya Singida. 

Kwa upande wake  Mkurugenzi wa Manispaa ya Singida  Zefrin  Lubuva alisema kuwa  Halmashauri ya Manispaa  ilipokea maagizo ya Mkuu wa Mkoa  ya kusafisha fukwe  za maziwa yote.

" Sisi Halmashauri ya Manispaa ya Singida pamoja na wananchi  tulipokea  maagizo yako na tunashukuru kwa kutuzindulia kampeni hii ya usafi wa mazingira   na maono yako ya Singida  safi inawezekana yatatimia",alisema  Lubuva"

Aidha Mkuu wa Mkoa  wa Singida Dkt. Binilith Mahenge   wakati akizindua kampeni hiyo alimuagiza Mkurugenzi wa Halimashauri ya Manispaa ya Singida kusimamia sheria ndogo kwa wale watakao ingiza mifugo katika maziwa hayo.

"Mkurugenzi kuanzia leo ni marufuku watu kuingiza ng'ombe kuona ng'ombe kuzagaa kandokando ya maziwa yetu kwa sababu taratibu unazo  wewe ni kuwatwanga faini tu  hatutaki kuona mifugo kwenye maziwa yetu",alisema Mahenge"

Alisema kuwa maziwa hayo ni chanzo kizuri cha mapato  kwa wale watakao kaidi agizo hilo ni kupigwa faini ya shilingi elfu hamsini  huku elfu kumi ikibaki wa mgambo na elfu 40 kuingia kwenye mapato ya Halmashauri.

Aliongeza kuwa  ni marufuku kwa wananchi kujenga vyoo ndani ya mita 60 kutoka kwenye ziwa ili kutunza mazingira na usafi wa maziwa  pamoja na walaji wa samaki wanaopatikana katika maziwa hayo.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments