HOSPITALI YA WILAYA KARAGWE YAKAMILIKA KWA 98%

SERIKALI ya Chama cha Mapinduzi (CCM) imetumia sh. bilioni 1.8 kujenga majengo mbalimbali ya hospitali ya wilaya ya Karagwe ambayo yamekamilika kwa asilimia 98.

Hayo yamesemwa jana (Jumanne, Septemba 29, 2020) na Mjumbe wa Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya Chama cha Mapinduzi (CCM) Kassim Majaliwa wakati akizungumza na wakazi wa kata ya Kayanga, katika mikutano uliofanyika kwenye uwanja wa Changarawe, wilayani Karagwe, mkoani Kagera wakati .

Akielezea ujenzi wa vituo vya afya kwenye wilaya hiyo, Mheshimiwa Majaliwa alisema sh. milioni 900 zimetumika kwa ajili ya ujenzi na ukarabati wa miundombinu mbalimbali ya vituo cha afya ambapo kati ya hizo, sh. milioni 500 zimetumika wa majengo ya kituo cha afya cha Kayanga ambapo kituo hicho kimekamilika na kinatoa huduma.

“Shilingi milioni 400 zimetumika kwa ujenzi wa majengo ya kituo cha afya cha Nyakayanja na ujenzi umekamilika. Pia shilingi bilioni 2.5 zimetumika kwa ajili ya ununuzi wa dawa, vifaa tiba na vitendanishi huku fedha za dawa kwa mwezi zilikuwa ni wastani wa shilingi milioni 53,” alisema.

Akielezea uboreshaji wa miundombinu kwenye wilaya hiyo, Mheshimiwa Majaliwa alisema uk. 74-76 wa Ilani ya uchaguzi ya CCM, unaelezea mpango wa Serikali kuanza ujenzi mpya (km 6,006.04) na ukarabati wa barabara kwa kiwango cha lami ikiwemo barabara ya Mugakorongo - Kigarama - Murongo yenye urefu wa km 105.

“Ilani yetu imeenda mbele zaidi na kuelezea mpango wa kukamilisha/kuanza upembuzi yakinifu na usanifu wa kina (km 7,542.75) barabara za mikoa kadhaa ikiwemo barabara ya Murushaka – Murongo yenye km 125.”

Mheshimiwa Majaliwa ambaye yuko mkoani Kagera kumuombea kura mgombea urais kwa tiketi ya CCM, Dkt. Magufuli alitumia fursa hiyo kumnadi mgombea ubunge wa jimbo la Karagwe, Bw. Innocent Bashungwa, mgombea udiwani wa kata ya Kayanga, na wagombea wa CCM wa kata za wilaya hiyo.

Alisema sh. bilioni 1.4 zimetolewa kupitia Wakala wa Barabara za Mjini na Vijijini (TARURA) kwa ajili ya kufungua barabara mpya, matengenezo ya kawaida, matengenezo ya sehemu korofi, muda maalum na makalvati. Alisema kati ya hizo, sh. milioni 585 zimetolewa kwa ajili ya matengenezo ya sehemu korofi na baadhi ya maeneo yaliyofanyiwa kazi ni ukarabati katika barabara ya Nyakagoyagoye-Karongo ambao uligharimu sh. milioni 31.

Akielezea ukarabati uliofanywa, alisema sh. milioni 19 zimetumika katika barabara ya Kanyabuleza-Runyaga; sh. milioni 14 zimetumika na katika barabara ya Mato-Karehe; sh. milioni 23 zimetumika katika barabara ya Kihanga - Rwabitembe – Mshabaiguru, sh. milioni 16 zimetumika katika barabara ya Nyakahanga – Kamahungu, sh.  milioni 16 zimetumika katika barabara ya Kishoju – Bujuruga na sh. milioni 23 zimetumika katika barabara ya Igurwa-Kibona-Nyakahita.

Alizitaja barabara nyingine zilizofanyiwa ukarabati kuwa ni Katoju-Ihembe – Bisheshe iliyogharimu sh. milioni 98, barabara ya Kanyabuleza Jct-Makabulini iliyotumia sh. milioni 69, barabara ya KDVTC FADECO iliyotumia sh. milioni 73, barabara ya AMRI – CLASIC iliyogharimu sh. milioni 38 na barabara ya Rukore – Chanika iliyotumia sh. milioni 115.

Alisema TARURA ilifanya matengenezo ya madaraja na makalvati katika barabara za Katoju- Rugu - Ruhita (sh. milioni 17), Igurwa-Nyakashozi-Rwentuhe (sh. milioni13), Rukore - Chanika (sh. milioni 12), Rubale - Kibogoizi (sh. milioni 6) na barabara ya Kasheshe - Rubare (sh. milioni 7).

“Shilingi milioni 124 zimetumika kwa ajili ya matengenezo maalum katika barabara za Kajunguti - Rubare - Misha (km. 9), Nyabiyonza-Kafunjo (km. 6), Kibaoni Nyabiyonza Sec - Kakuraijo (km. 3.15), Nyakakika - Kandegesho (km.5), Lukole - Kigarama, Lukoyoyo – Kantabire -Nyakasimbi na Ahamulama – Busecha,” alisema.  

 


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments