HALMASHAURI ZATAKIWA KUTENGA ARDHI YA KILIMO KWA AJILI YA VIJANA


Naibu Waziri wa Kilimo Omary Mgumba ameziagiza halmashauri zote nchini kutenga ardhi ya kutosha kwa ajili ya vijana kuzalisha mazao ya kilimo,mifugo na uvuvi.

Ametoa agizo hilo leo mjini Njombe wakati alipofungua kongamano la vijana wa mikoa ya Njombe,Ruvuma na Iringa kujadili fursa zilizopo katika sekta ya kilimo nchini.

Mgumba amesema kumekupo na malalamiko ya vijana kukosa ardhi kutokana na halmashauri kuwa na mashamba pori mengi yasiyopimwa na kulimwa.

“Halmasahauri zote zihakiki mashamba pori yote au yaliyochukuliwa mikopo na hayalimwi yapimwe na kugawiwa kwa vijana walio tayari kufanya kazi za kilimo nchini”.alisema Naibu Waziri Mgumba.

Ili kufanikisha hilo Mgumba mewataka vijana kujisajili kwenye daftari la wakulima linaroratibiwa na wizara yake ili serikali iwatambue na kujua changamoto zao na kisha kuwaonyesha fursa za ajira kwenye kilimo.

Naibu Waziri Mgumba amesisitiza halmashauri nchini kutoa fedha za mikopo kwa vijana bila urasimu ili vijana wanufaike na kuanzisha kazi za uzalishaji mazao ya kilimo na mifugo.

Mgumba aliwafahamisha kuwa serikali imeelekeza Benki ya Maendeleo ya Kilimo (TADB) kuendelea kutoa mikopo kwa vijana ili wapate mitaji.

“Wapo vijana wengi wasomi wameamua kujiajili katika kilimo ili kufikia malengo ya kuongeza ajira ikiwa ni malengo ya Serikali ya Awamu ya Tano kukuza sekta ya kilimo” alisema Mgumba.

Tanzania ina eneo la hekta milioni 44 zinazofaa kwa kilimo hivyo vijana wajitokeze kutumia fursa hiyo kuanzisha kazi za kuzalisha mazao ya kilimo .

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Njombe Ruth Msafiri aliyemwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Njombe aliziagiza halmashauri zote za mkoa wa Njombe kuandaa katiba kwa
ajili vijana kushiriki shughuli za kilimo.

Aliongeza kusema watendaji wote wa halmashauri wapunguze urasimu kwa kukaa muda mrefu bila kupitisha maombi ya vijana wanaostahili mikopo ya fedha za mapato
ya ndani.

“Halmashauri punguzeni urasimu msikae zaidi ya robo mwaka bila kutoa mikopo kwa vijana,akina mama na walemavu” alisema Mkuu huyo wa wilaya ya Njombe.

Naye Mkurugezi wa Shirika la SUGECO Revocatus Kimario linaloratibu mafunzo maalum kwa vijana kwenda Israel na Marekani kujifunza fursa za kilimo kwa vitendo kwa mwaka mmoja amesema wengi wamenufaika.

Kimario amesema hadi sasa zaidi ya vijana 1000 wamepatiwa mafunzo ya kilimo,mifugo na uvuvi nchini Israel na wengine 90 nchini Marekani wamerudi nyumbani
wamefanikiwa kuzalisha ajira nyingi kwa wenzao .

Kimario ameishauri jamii kutotumia kilimo kama adhabu bali kitumike kama fursa ya kukuza ajira na kipato cha kaya na taifa.

Kongamano hilo la siku mbili linawakutanisha vijana wapatao mia mbili toka mikoa ya Njombe,Ruvuma na Iringa chini ya uratibu wa Wizara ya Kilimo na wadau toka wizara za kisekta na taasisi binafsi.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527