KUHUSU BIBI ANAYEDAIWA KUWA MCHAWI KUKUTWA AKIWA UCHI NYUMBANI KWA MTU MJINI SHINYANGA

Bibi kizee anayekadiriwa kuwa na umri wa miaka (70), asiyejulikana jina wala makazi yake,ameanguka akiwa uchi wa mnyama kisha kuanza kutembea kwa kutumia makalio nyumbani kwa Suzana Mwandu mkazi wa mtaa wa Mageuzi manispaa ya  Shinyanga mkoani Shinyanga, wakati akiwa katika safari zake kwa kile kinachodaiwa kuwa ni imani za kishirikana.



Akielezea tukio hilo juzi mama mwenye nyumba alikonasa kikongwe huyo bibi Mwandu  alisema majira ya saa moja asubuhi Januari 29 mwaka huu, alipoamka kuwaamusha wajukuu zake waende shule, ndipo alipomkuta kikongwe  akiwa amelala uchi wa mnyama  nje ya nyumba yake.


Bi Mwandu alisema, baada ya kikongwe huyo kuanguka alijivuta ndani ya jiko lake lililoko nje ya nyumba ambalo lipo wazi, na baada ya kuanza kumsemesha ndipo kikongwe  akazinduka na kuanza kuongea maneno ya ushirikina, hali ambayo ilimtia wasiwasi na kutoa taarifa kwa uongozi wa serikali ya mtaa.

“Nyumba yangu nimeizindika vilivyo, hivyo kikongwe huyu alipokuwa katika safari zake na kupita maeneo ya nyumbani kwangu ndipo akakutana na balaa hilo na hatimaye akajikuta ameanguka na kujivutia ndani ya jiko  kwa ajiri ya kujistiri” alisema Bi Mwandu.

“Unajua siku zote mchawi anapoanguka  na ukimwacha kwa muda mrefu bila ya kumsemesha, anaweza kupoteza maisha, hivyo kutokana na mimi kutokuwa na ubaya naye nikaona bora nimusemeshe, ili kumuokoa, na baada ya hapo  nikampa nguo za kujistili na aibu ya kuwa mtupu”,aliongeza  Bi Mwandu.

Kwa upande wao mashuhuda wa tukio hilo waliiambia malunde1 blog kuwa bibi huyo huenda akawa ni mchawi kutokana na kauli zake tatanishi na maneno ya kichawi aliyokuwa anayatamka huku mikono yake ikionekana kukatwa kwa mapanga na kuota sugu.

Walisema kikongwe huyo alikuwa haongei na alikuwa hawezi kusimama na badala yake alikuwa anatembelea makalio yake kutokana na kukosa nguvu.

“Huyu bibi atakuwa mchawi angalia hata mikono yake imekatwa katwa na imekomaa kweli huenda huwa anajigeuza fisi na kutembelea mikono,halafu macho yake siyo ya kawaida,ana kiburi kupita kiasi na ndiyo tabia za wachawi wengi”,alieleza Halima Juma.

“Bibi huyu kafanya vituko,katoa pesa shilingi hamsini,mia mbili,mia tano na elfu moja kutoka kiunoni mwake akaanza kuzirusha na ndipo kapata nguvu hata za kusimama,atakuwa kazidiwa nguvu,kapita anga mbaya”,Hamis Mayunga aliiambia Malunde1 blog.

Naye mjumbe wa serikali ya mtaa wa Mageuzi Waziri Mussa(Chadema) alikiri kuwepo kwa tukio hilo ambalo lilijaza umati wa watu, huku wakishindwa kumtambua kikongwe huyo wapi alikuwa akitoka wala anapokwenda kutokana na maswali waliyokuwa wakimuuliza na kushindwa kuongea maneno sahihi zaidi ya yale ya ushirikina.

Hata hivyo Mussa alisema, wakati wakiendelea kumuhoji ndipo bibi huyo alipozidi kupata fahamu ambapo pia walimpatia uji ili kupata nguvu, lakini kutokana na kutomtambua na kushindwa kuelewana ili bidi aongee na wanazengo akawasihi wasimdhuru na kuita jeshi la polisi.

Jeshi la polisi lilifika eneo la tukio na kumkuta bibi huyo tayari ameanza kupata nguvu kisha kuwaomba wakazi wa eneo hilo wamuache kikongwe huyo aendelee na safari zake kutokana na kwamba serikali haimini uchawi.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527