
Wafanyakazi wa Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) wameungana na wafanyakaz wengine duniani kote kuadhimisha Sikukuu ya Wafanyakazi Duniani (Mei Mosi) ambapo maadhimisho haya kitaifa yamefanyika katika viwanja vya Lunyanywi, Halmashauri ya Mji wa Njombe.
Maadhimisho haya yalikuwa na kauli mbiu ya "Kazi zenye Staha ni Nguzo Imara Kwa Maendeleo Endelevu Katika Utekelezaji wa Dira ya Taifa 2050"
Akizungumza katika maadhimisho hayo, Afisa Rasilimali Watu Mwandamizi wa STAMICO, Bi Leah Jericko amesema ushiriki wa STAMICO kitaifa na kwenye Mikoa ni ishara ya kuthamini mchango wa wafanyakazi katika maendeleo ya taifa pamoja na kutambua nafasi zao katika kukuza sekta ya madini nchini.
Aidha, amelishukuru Shirika kwa kuwawezesha wafanyakazi kushiriki katika maadhimisho hayo kitaifa na kwenye Mikoa Mbalimbali na ametoa wito kwa watumishi wote kuendelea kufanya kazi kwa bidii, weledi na uzalendo ili kuhakikisha STAMICO inafikia malengo iliyojiwekea.
Kwa upande wake, mfanyakazi Hodari wa STAMICO, mwaka huu wa 2026, Bwn Mark Magessa ameushukuru Uongozi na Watumishi wenzake kwa kumuona anafaa kupata tuzo hiiyo na amesema kuhudhuria Maadhimisho haya kumewapa fursa ya kujifunza mambo mbalimbali, kubadilishana uzoefu na kujenga mshikamano na wafanyakazi kutoka taasisi nyingine.
Maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi Duniani hufanyika kila mwaka Mei Mosi kwa lengo la kutambua mchango wa wafanyakazi katika maendeleo ya jamii na taifa kwa ujumla.
STAMICO imeshiriki Maadhimisho hayo kitaifa Mkoani Njombe sambamba na ofisi zake zote katika mikoa ya Dar es Salam, Dodoma, Singida, Geita na Songwe.






Social Plugin