BINTI AFARIKI AKIFANYIWA MAOMBI NYUMBANI KWA MCHUNGAJI


Binti mmoja mkazi wa Magamba Kijiji cha Mkuyuni Halmashauri ya Manispaa ya Mpanda mkoani Katavi, Consolata Charles (16) amefariki dunia nyumbani kwa Mchungaji wakati akiombewa.

Kwa mujibu wa baba mlezi, Charles Gasto na mama mlezi wa marehemu wamesema binti huyo alikumbwa na hali ya kutokwa damu puani na vidonda mdomoni ghafla na baada ya siku chache alizidiwa na kukimbizwa Hospitali ya Manispaa ya Mpanda kwa matibabu zaidi.

Wamesema, baada ya vipimo hospitalini aligundulika kuwa na ugonjwa wa Malaria na UTI ndipo alipopewa dawa kabla hajaruhusiwa kurudi nyumbani baada ya kupata nafuu ambapo siku chache baada ya kuruhusiwa alizidiwa tena.

Alipozidiwa tena ndipo waumini wa kanisa lake (walokole) walimchukua ili wakafamfanyie maombi kabla umauti haujamfika akiendelea kuombewa.

Mchungaji wa Kanisa hilo aliyekuwa akimfanyia huduma ya maombezi, Peter James amesema kama Kanisa walipokea simu kutoka kwa familia ya marehemu wakiomba msaada kutokana na hali ya kimaisha kuwa duni na mgonjwa hakuwa na uangalizi mzuri ndipo walipokubaliana akafanyiwe maombezi.

Marehemu Consolata Charles alifikwa na umauti Machi 4, 2023 na amezikwa katika makaburi ya kijiji hicho.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments