KINGI AFARIKI BAADA YA KUCHANGANYA POMBE KALI



Makasi Kingi (37)


Makasi Kingi (37) mkazi wa mtaa wa Tambukareli Kata ya Butimba wilayani Nyamagana jijini Mwanza, amefariki dunia baada ya kunywa pombe aina ya gongo iliyokuwa imechanganywa na K-Vant huku akidaiwa kunywa pombe hizo bila kula chakula chochote.

Taarifa iliyotolewa na Jeshi la Polisi imeeleza kwamba tukio hilo limetokea Februari 19, 2023 majira ya saa 2:00 katika mtaa huo Kingi alikuwa anakunywa pombe aina ya gongo ambayo alichanganya na K-vant akiwa na wenzake wawili na kupelekea kifo chake.

Kupitia taarifa aliyoitoa Kamanda wa Polisi mkoa wa Mwanza Wilbroad Mutafungwa, amesema hadi sasa wanawasaka watu hao wawili ili waweze kuwahoji kuhusu tukio hilo, ambapo EATV haikushia hapo ikafika hadi katika mtaa wa Tambukareli na kufanikiwa kuzungumza na wake wa marehemu ambao wamesema wamepokea kwa masikitiko taarifa ya kifo cha mume wao huyo huku wakisema alipotoka nyumbani alikuwa mzima wa afya.

Kwa upande wa Mwenyekiti wa chama cha Makondakta Jijini Mwanza Hassan Amini amesema chama chao kimepoteza mtu muhimu kwani alikuwa mpambanaji.

"Tumepokea kwa masikitiko taarifa ya kifo cha mwenzetu, sababu alikuwa kijana menzetu na tulikuwa tunaendelea na shughuli zetu ndani ya usafirishaji katika mkoa wa Mwanza kwa taarifa tuliyoipata kwamba amefia sehemu ya starehe tunachomuombea kwa mwenyezi Mungu ampokee kwani yeye ametangulia na sisi ni wafuasi wa baadae," amesema Amini.

CHANZO - EATV

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments