MAJAMBAZI WAVAMIA KAMBI YA WACHINA WANAOJENGA RELI YA KISASA OLD SHINYANGA, POLISI WADAKA 9


Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga ACP Janeth Magomi akionesha bunduki iliyotumika katika tukio la ujambazi kambi ya Wachina wanaojenga mradi wa Reli ya Kisasa eneo la Old Shinyanga


Na Kadama Malunde & Halima Khoya - Malunde 1 blog

Jeshi la polisi mkoa wa Shinyanga linawashikilia watuhumiwa 9 wa ujambazi wanaodaiwa kuvamia Kambi ya Raia wa China wanaojenga reli ya Kisasa (SGR) katika eneo la Old Shinyanga mkoani Shinyanga.


Akitoa taarifa kwa vyombo vya habari leo Jumatatu Februari 6,2023 Kamanda wa Polisi mkoa wa Shinyanga ACP Janeth Magomi amesema wamewakamata watuhumiwa tisa wa ujambazi ambao walihusika katika tukio la ujambazi lililotokea Februari 4,2023 katika kambi ya Wachina wanaojenga reli ya kisasa katika eneo la Old Shinyanga.


“Katika ukamataji huo pia tulifanikiwa kukamata Bunduki aina ya Shortgun Pump Acrtion iliyotumika katika tukio hilo la ujambazi pamoja pesa za nchi mbalimbali zikiwemo Naira 16,000 za Nigeria, Dollar 100,500 za Vietnam, Yuan 20 za China, Dinar 1.5 za Kuwait na Rial 900 za Cambodia”,ameeleza Kamanda Magomi.


Amesema jeshi la polisi pia limekamata lita 910 za mafuta aina ya diesel yanayotumika katika mradi wa Reli ya Kisasa Old Shinyanga na pikipiki 8 madumu ya kubebea mafuta na mipira ya kunyonyea mafuta ambavyo vilikuwa vinatumika katika uhujumu uchumi katika mradi huo wa SGR.


“Jeshi la polisi mkoa wa Shinyanga linawataka wananchi hususani vijana kuacha tabia ya kujihusisha na vitendo vya uhalifu na pia kuacha kabisa kufanya hujuma kwenye mradi wa reli ya kisasa kwa serikali ya awamu ya sita imedhamiria kuwatumikia wananchi wake kwa kuwajengea miundombinu madhubuti na hivyo inahitaji kuungwa mkono katika juhudi hizo”,amesema Kamanda Magomi.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga ACP Janeth Magomi akizungumza na waandishi wa habari
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga ACP Janeth Magomi akionesha bunduki iliyotumika katika tukio la ujambazi kambi ya Wachina wanaojenga mradi wa Reli ya Kisasa eneo la Old Shinyanga
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga ACP Janeth Magomi akionesha fedha za kigeni zilizokamatwa
Fedha za kigeni zilizokamatwa
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Shinyanga ACP Janeth Magomi akionesha madumu ya mafuta yaliyoibiwa kwenye mradi wa Reli ya Kisasa maeneo ya Old Shinyanga.

Picha na Kadama Malunde - Malunde 1 blog


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments