KUWA MSIRI MAMBO YAKO YASIHARIBIKE TENA 2023

 

Ingia 2023 na Siri ya kutunza Siri ili Malengo Yako Yasiharibe Tena

Mafanikio ni siri. Watu wakijua siri za mipango yako watakutoboa macho usione mafanikio yako kama Samson. Samson alitobolewa macho baada ya kushare siri zake na Delila.

Imeandikwa katika Biblia Takatifu kwamba hata mwanamke anayelala kifuani kwako asijue siri zako (Mika 7:5-6). Unaona mambo hayo?

Yusufu aliuzwa na ndugu zake kwa sababu ya kuropoka ndoto zake hovyo. Sasa washirikishe wazazi wako ndoto zako wakawatambie majirani zenu uone kama utatoboa!

Ulisema 2022 ni mwaka wako lazima ununue gari, mwaka wako umeisha hata tolori huna. Unaumia sana konda anavyokwambia kaa chini trafiki asikuone! Wewe kweli ni wa kuambiwa kaa chini!

Ulisema 2022 ni mwaka wako lazima uhamie kwenye nyumba yako, ukaishia kumwaga mchanga site. Sasa unaogopa hata kwenda site. Hata picha za ujenzi hupost tena.Jamanii!

Ulisema 2022 ni mwaka wako lazima ufunge ndoa lakini mwaka wako umeisha na mchumba ndo kwanza hasomeki. Hata online haonekani na wakati alikuwa anashinda huko. Sijui kakublock Mungu wangu!! Sasa kwa nini na wewe ulitangaza?

Ulisema 2022 ni mwaka wako lazima ufungue duka lakini mwaka unaisha huna hata hamu ya kufanya biashara. Hata mkopo uliochukua umeula. Unachenga kuulipa.Taabu tupu!

Ulisema 2022 ni mwaka wako lazima
uende shule, ukamtangazia kila mtu, ukaishia kujaza fomu tu. Ziko mezani kwako! Ukiziona unamind. Wenzako waliokwenda shule ukiwaona roho inaumaaa!

Ulisema 2022 ni mwaka wako lazima
uanze ufugaji wa kuku wa mayai, uliowatangazia wakakukomesha, ukaishia kujenga mabanda. Yerewiiii!!

Ulipandishwa cheo, ukashushwa kwa sababu ulishindwa kutunza siri. Labda nikwambie, hata kama una akili nyingi kiasi gani huwezi pewa nafasi za maana kama huna siri.

Huwezi kuwa Nabii Mkuu kama huna siri; huwezi kuwa Daktari Bingwa kama huna siri; huwezi kuwa Tajiri Mkubwa kama huna siri, huwezi kuwa Mwandishi Nguli kama huna siri!

Nimekusikia tena umeanza kutangaza kwamba 2023 ni mwaka wako. Tayari umejiwekea malengo mengine ili yakabume tena maana bado hujaacha kumwaga mchele kwenye kuku wengi. Friji haligandishi. Bado unaongea mnooo!

Mwaka 1926, Kurt Lewin, Baba wa Saikolojia, alisema unapotangaza mipango yako unaifanya akili ione kama tayari limeishafanyika na hivyo kukosa hamu ya kufanya.

Umetangaza mwaka huu lazima usome vitabu vya kutosha mara unashangaa kila ukishika kitabu unaishiwa hamu ya kusoma, unaacha. Mwaka unaisha hujasoma.

Ukianza kutekeleza jambo unajisikia uvivu kweli. Uvivu ni kupumzika kabla ya kuchoka.

Usipotunza siri zako, 2023 utapita tena kapa nakwambia. Bila kutunza siri kila kitu kitakuwa kigumu kwako. Hata ndoa itakuwa ngumu.Utauchukia mwaka nakwambia.

Unatakiwa kuelewa kwamba siyo kila unayemshirikisha mipango yako akasema hongera ukadhani inatoka moyoni. Wengine zinatoka mdomoni, moyoni inatoka "ushindwe." Na akishasema ushindwe unashindwa kweli.

Kuna mtu utamuona dhaifu kwa macho lakini katika ulimwengu wa roho ana mamlaka makubwa ya kuzuia mipango yako. Ndiyo maana ni hatari kuwa na marafiki wengi maana wakiona unaelekea kuwashinda wanakimbia kukuvuta shati huko kwenye ulimwengu wa roho.

Kumbuka mambo yote yanaanzia huko kwenye ulimwengu. Kwani hujawahi kuota ajali imetokea na kweli ikatokea? Sasa ile siyo ndoto. Ule ni uhalisia, uko kwenye ulimwengu wa roho, au tuseme ulimwengu wa akili.

Jifunze kufanya mambo yako kuwa siri.
Ni utukufu wa Mungu kuficha jambo (Mithali 25:2). Hata sadaka yako iwe kwa siri. Hakikisha mkono wako wa kushoto usijue ufanyalo mkono wako wa kuume. Baba yako aonaye sirini atakujazia.

Siri ni ulinzi. Mtu asiye na siri hana ulinzi. Kazi ya siri ni kufanya mambo yako yaende kama ulivyopanga. Usirudie kosa mwaka 2023. Siri ipo kwa ajili ya mafanikio.

Matajiri wote wanaficha mipango yao. Tunawaita washirikina kwa sababu ya usiri wa mambo yao. Na kama unavyojua tena, jamii yetu watu wasipokujua, watakupa utambulisho mbaya ili uropoke siri zako.

Utasikia anauza watu; anakunywa damu; analala makaburini utadhani ulilala naye. Lakini matajiri hawadanganyiki. Waite majina yote lakini hutoona wakijibu ng'oo!

Utajiri ungekuwa ni ushirikina basi Sumbawanga, Kigoma na Pemba pangekuwa kama Ulaya. Wachawi wamenielewa.

Tajiri atakwambia "nilinunua basi nikiwa na umri wa miaka 19 na pesa sikurithi kutoka kwa mtu yoyote;" lakini kamwe hatakwambia alinunuanunuaje!

Maskini unaweza kukutana naye leo akakusimulia hadi idadi ya vichaa katika ukoo wake utadhani kaulizwa. Sasa kwa hadithi mbaya kama hizi nani atakupa mchongo?

Waliovumbua ndege hawajatoa siri hadi leo. Jifunze kwa hao. Acha kujianika. Hata kama una mpango wa kufuga kuku usiwaambie watu, anza kimyakimya washitukie unauza mayai. Ukianza kutangaza hutofuga, na ukifuga watakufa. Nani kawaua? Utajua hujui.

Usiwaonyeshe watu ng’ombe anayekupa maziwa,watampa sumu ukose maziwa. Kumwambia mtu mipango yako kabla ya kutenda ni kutoa siri! Hii imewagharimu watu wengi. Ficha mipango yako; fichua matokeo.

Siri ni hatima ya maisha yako. Coca cola ingetoa siri zake isingekuwa namba moja kimauzo duniani kwa vinywaji baridi. Utamu wa kuku kwenye migahawa ya KFC kote duniani imebaki kuwa siri tangu mwaka 1930 ugunduliwe na Herland huko Kentucky.

" Man is not what he thinks he is, he is what he hides ," alisema André Malraux. Maisha ni siri. Wazungu wamefanikiwa sana katika hili. Mpaka leo siri za kutengeneza ndege zimebaki mikononi mwao. Utatengeneza ndege lakini haitaruka.

Wazungu wameunda mpaka jamii za siri. Wanaziita Secret Society. Hawa ndo wanatawala dunia. Ni muunganiko wa familia 13 tu, google utazijua.

Wametengeneza historia ya dunia kutuaminisha kwamba hatuwezi kufanikiwa bila kutegemea huruma za Mungu. Na kweli kila kinachotokea tunasema ni mipango ya Mungu.

Hata mtu akifa kwa kula kinyesi tunasema ni mpango wa Mungu. Kwani kipindupindu si ugonjwa unaosababishwa na kinyesi?

Wametutengenezea skripti za maisha kama wasanii. Hatutakiwi kutoka nje ya hizo skripti, tutaharibu muvi na director atachukia. Ndani ya hizo skripti za maisha tumeambiwa kuoa wake wengi ni dhambi lakini nje ya hizo skripti mtu anamichepuko ya kutosha. Hapa nature inataradadi.

Leo ukimwambia Mswahili unaweza kuongea na Mungu bila kupitia dini yoyote hawezi kukuelewa. Ukimwambia Mungu ni mkubwa sana kuliko walivyotufundisha kupitia dini utaambiwa una kufuru.

Tumepandikizwa ujinga kwamba vitu vizuri vyote ni vya shetani.

Halafu hawa secret society walivyo wajanja, hawaruhusu watoto wao kuoana na watu wa kawaida.Wanawachagulia watoto wao wachumba. Sisi tukifanya hivyo tunaambiwa ni ushamba. Matokeo yake watoto wetu wanaingia kwenye ndoa na mijitu ya ajabu. Lengo ni kutuvuruga.

Halafu wako serious sana katika hilo. Mtoto atakayekaidi wanamuua. Kilichomtokea Princess Diana baada ya kumpenda Dodi Fayed kijana wa Uswahilini wote tunajua. Sasa wametuletea ushoga na wakati wao hawafanyi kabisa.

Mafanikio ni mchezo wa kuangushana, ukiweza kutunza siri huwezi kuangushwa.

Kwahiyo kabla hujaanza safari ya kutimiza malengo yako ya mwaka 2023, anza na safari ya kutunza siri.

Huna siri unaonekana mtu wa hovyo sana. Mungu mwenyewe mambo kibao ameyafanya siri, wewe ni nani unaropoka kila unachokifanya. Ndiyo, kwani nani aliishamuona Mungu? Hata kifo Mungu ameendelea kukifanya siri. Hakuna anayejua atakufa lini.

Siri ni maisha. Vitu vyote vya thamani na vitamu vimewekwa sehemu za siri. Siri huwa haisemwi. Siri inatekelezwa.

Kwa nini Mungu alikuwa anaongea na Musa peke yake na kumpa maagizo akiwa peke yake? Siri!

Herode alishindwa kumuua Yesu kwa sababu wazazi wake walifanya siri. Mwenzangu ukipata mimba unatembea unatema mate njia nzima, unapiga picha tumbo na vichupi unashare. Huyo mtoto unamuweka hatarini.

Siri ni msingi wa maisha.Hata maisha ya ndoa yana siri zake; usidhani ni uvumilivu tu. Kuna waliovumilia wakafia humo. Waulize walidumu watakwambia.

Usijitenge na watu lakini watenganishe watu na siri zako. Kitu chochote cha thamani kimejificha. Msanii anayeonekana hadharani kila mara anapoteza thamani.

Hata Mungu angekuwa anaonekana mitaani kuna wapuuzi wangemzoea na kumchukulia poa.

Moyo ni wa thamani ndiyo maana umefichwa. Mipango yako ni ya thamani ifiche. Kuitangaza inaishiwa thamani. Premature announcements attracts evil spirits. Acha kupiga mayowe: subiri wayaone wenyewe. Michongo mingi huharibika unapoisema.

Usiri ni hatua muhimu sana kuelekea kwenye mafanikio. Ukianza kutunza siri zako mambo mengi yatanyoka na mwaka 2023 utakuwa mwaka wa baraka kwako.

Utajiri hupenda watu wenye tabia ya kujificha. Utajiri unahitaji usiri; umasikini unahitaji uwazi uchaguzi ni wako. Tajiri hapendi aonekane ana pesa kama maskini.

Masikini atafanya hivyo kwa kuvaa vizuri kwa sababu kuvaa vizuri kunaficha umaskini. Matajiri wanaficha utajiri kwa kuishi kimaskini, maskini anaficha umaskini kwa kuishi kitajiri!

Ni hatari kuishi kitajiri na wakati unafikra za kimaskini kichwani. Ingia mwaka 2023 na fikra za kitajiri.Kanyaga mwaka 2023 kwa maringo na mbwembwe maana siri umeijua.

MWISHO.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments