MRADI WA MAJI WA SH.BILIONI 1.6 KWENDA KUMALIZA CHANGAMOTO YA MAJI HIFADHI YA TAIFA RUAHA

Na Mwandishi Wetu, Michuzi TV- Ruaha

HIFADHI ya Taifa ya Ruaha imesema kwa sasa kuna mradi mkubwa wa maji ambao unaendelea katika eneo la Malumbe Kijiji cha Tungamalenga kwa lengo la kuhakikisha maji hayo yanafika kwenye eneo la ndani ya hifadhi hiyo, ili kuondokana na adha ya kukosa maji safi na salama.

Imeelezwa kwamba ili kufanikisha mradi huo kiasi cha Sh.bilioni 1.6 kimepangwa kutumika kuanzia mwanzo wa ujenzi hadi kukamilika kwake na kwamba ulianza Septemba na unatarajia kukamilika Desemba mwaka huu na hivyo kutaondoa adha ya kukosekana kwa maji safi na salama iliyoko kwa muda mrefu.

Akizungumza na waandishi wa habari Kamishna Msaidizi wa Uhifadhi,Mkuu wa Hifadhi ya Taifa ya Ruaha Godwell Ole Meing’ataki amesema kuwa kwa sasa wanaendelea na ujenzi wa mradi mkubwa wa maji ambao unatekelekezwa kwa ushirikiano wa Hifadhi ya Taifa ya Ruaha pamoja na wananchi wa Tungamalenga na Msembe na maji hayo yatakwenda ndani ya hifadhi hiyo.

“Maji haya yanaelekea katika Hifadhi ya Taifa ya Ruaha hasa eneo la Msembe lakini pia maji haya yatapelekwa kwenye tenki lililopo Kingamalenga kwa ajili ya jamii ya watu wa pale , ikumbwe kwamba Hifadhi ya Taifa ya Ruaha kwa miaka 58 tangu ianze kumekuwa na changamoto kubwa ya maji na maji yaliyokuwepo katika eneo hili hayana ubora na sio salama , mara nyingi haya maji hayafai kwa ajili ya kupikia , kunywa kwani ni maji ambayo yana chumvi chumvi hata ukijaribu kuoga hautakati hata ukitumia sabuni maji haya hayafai.

“Na pia viwango vya madini mbalimbali kwenye maji haya yako juu na sio mazuri haishauri kwa binadamu kunywa wala kupikia.Hata ukitaka kupikia utakuta sufuria inabadilika kutokana na chumvi nyingi, sasa Hifadhi yetu ya Taifa ya Ruaha kwa kushirikiana na kijiji cha Kingamalenga walibuni mradi huu na sasa utakwenda kuhakikisha uhakika wa maji safi na salama yanapatikana katika kijiji cha Msembe kwa ajili ya matumizi ya watumishi ,familia zao lakini na idadi kubwa ya wageni ambao wanatembelea hifadhi ya taifa ya Ruaha

“Huu mradi umetoka hapa mpaka Hifadhi ya Taifa ya Ruaha eneo la Msembe takribabani kilometa 36, mitaramo na mabomba yameshatandazwa katika kilometa hizo , kazi ambayo inafanyika hapa ni kujenga eneo la dakio la maji na baada ya hapo tutaunganisha mabomba na kupeleka maji eneo la Msembe.Pia tumejenga tenki kubwa kwa ajili ya kutunza haya maji halafu tutakwenda kuyasambaza hadi hifadhini,”amesema.

Hivyo amesema kwa hiyo mradi huo ni wa kipekee ambao unaonesha manufaa ya ushirikiano kati ya wananchi wanaoishi jirani na hifadhi kwani bila ya mahusiano mema kati yao na wananchi wasingeruhusiwa kuchukua maji ambayo hata wao wananchi wanayahitaji.Pia wasingeruhusu mitaro na mabomba kupita kwenye mashamba yao, maeneo ya makazi kwa ajili ya kupela maji kwenye Hifadhi ya Taifa Ruaha.

“Tunashukuru kwa ushirikiano ambao tumeupata na huu ni mradi mkubwa ambao unakwenda kunufaisha hifadhi lakini na wananchi nao kwa upata maji safi na salama, huu mradi ni mkubwa na umetumia takribani Sh.bilioni 1.6 ambazo ndio zimetumika kwenye huu .Lakini kubwa zaidi katika kipindi cha kutekeleza mradi wananchi hawa wamekuwa waaminifu.Tunachohurahia maji yapo ya kutosha.

Kwa upande wake Ofisa Uhifadhi wa Taifa Ruaha Kitengo cha Uhusiano kwa Jamii Priscus Mrosso amesema hifadhi hiyo makao makuu yake yapo Msembe ambacho ni kitongoji cha Kijiji cha Kingamalenga kwa hiyo wameuchukua mradi huo katika Kijiji cha Malunde.“Ni sehemu ya ujirani mwema na ni mradi ambao unakwenda kutunufaisha sisi wote.

“Kwa awamu hii ambayo mradi unatekelezwa sasa hivi Tungamalenga watapata maji kidogo lakini kwenye awamu ya pili ya mradi ambayo hayajatolewa la maji lakini awamu ya pili watapata maji mengi , kwani tutaongezea nguvu kwenye tanki lao kubwa la maji ambalo liko hapa kwenye kijiji. Mahusiano kati ya hifadhi na kijiji cha Kingamalenga yako vizuri ndio maana waliliridhia hifadhi kupitisha mabomba katika maeneo yao ya mashamba, pia waliahidi mabomba hayo watayalinda kwani wanajua watanufaika na hayo maji ambayo yanatakiwa kutoka Kijiji cha Malumbe mpaka hifadhini,”amesema.

Wakati huo huo Ofisa Mtendaji Kijiji cha Tungamalenga Linuss Mweluka amesema mahusiano kati yao,TANAPA na Hifadhi ya Taifa ya Ruaha hayajaanza leo ni muda mrefu na wamekuwa wakipata wa kujengewa majengo mbalimbali taasisi hasa Elimu na Afya .

“Lakini kwa mradi huu wa maji tunasema umefika kwa wakati kwasababu kijiji chetu kilikuwa na changamoto sana ya maji ya bomba , kwa mahusiano tuliyonayo na TANAPA hadi sasa tumeshaambiwa tunaletewa maji hayo na tutawekewa kwenye tenki ambalo lipo hapa kwa ajili ya kutumia sehemu kubwa kwa taasisi mbili elimu na afya kwa awamu hii ya kwanza

“Kwa awamu ya pili tutatoa maombi kwa ajili ya huduma kwa ujumla ya kijiji kizima kwa hiyo kwa niaba ya wananchi na Serikali ya Kijiji cha Kinamalenga napenda kutoa shukrani zangu za awali kwa TANAPA , ahadi yetu sisi ni kutoa ushirikiano hasa katika ulinzi wa mradi kwasababu mara nyingi kwenye miradi kama hii ya maji ambapo kumepita mabomba huwa kunatokea uharibifu lakini tumejipanga ili kulinda vizuri mradi huo.”

Kuhusu ushiriki wao kwenye kulinda hifadhi hiyo amesema kupitia elimu ambazo zimekuwa zikitolewa wananchi wamekuwa na uelewa mkubwa kuhusu umuhimu wa hifadhi na ndio maana hata ujangili kwa sasa umepungua.

Kamishna Msaidizi wa Uhifadhi,Mkuu wa Hifadhi ya Taifa ya Ruaha Godwell Ole Meing’ataki alipokuwa akizungumza mambo mbalimbali kuhusu hifadhi hiyo ukiwemo mradi mkubwa wa maji ambao unaendelea katika eneo la Malumbe Kijiji cha Tungamalenga mkoani Iringa kwa lengo la kuhakikisha maji hayo yanafika kwenye eneo la ndani ya hifadhi hiyo, Ambapo katika Mradi huo kiasi cha Sh.bilioni 1.6 kimepangwa kutumika kuanzia mwanzo wa ujenzi hadi kukamilika kwake na kwamba ulianza Septemba na unatarajia kukamilika Desemba mwaka huu na hivyo kutaondoa adha ya kukosekana kwa maji safi na salama iliyoko kwa muda mrefu.

Kamishna Msaidizi wa Uhifadhi,Mkuu wa Hifadhi ya Taifa ya Ruaha Godwell Ole Meing’ataki akiwa eneo unapojengwa mradi mkubwa wa maji ambao unaendelea katika eneo la Malumbe Kijiji cha Tungamalenga mkoani Iringa kwa lengo la kuhakikisha maji hayo yanafika kwenye eneo la ndani ya hifadhi hiyo, Ambapo katika Mradi huo kiasi cha Sh.bilioni 1.6 kimepangwa kutumika kuanzia mwanzo wa ujenzi hadi kukamilika kwake na kwamba ulianza Septemba na unatarajia kukamilika Desemba mwaka huu na hivyo kutaondoa adha ya kukosekana kwa maji safi na salama iliyoko kwa muda mrefu. PICHA ZOTE NA MICHUZI JR-RUAHA.

Ujenzi wa mradi mkubwa wa maji ambao unaendelea katika eneo la Malumbe Kijiji cha Tungamalenga mkoani Iringa kwa lengo la kuhakikisha maji hayo yanafika kwenye eneo la ndani ya hifadhi ya Taifa ya Ruahahiyo kuondokana na adha ya kukosa maji safi na salama.
Mmoja wa wakazi wa Kijiji cha Tungamalenga ambaye pia mmoja wa mafundi wanaoshiriki kwenye ujenzi wa Mradi huo akieleza manufaa makubwa watakayoyapata mara baada ya kukamilika kwa mradi huo,ambao pia utanufaisha vijiji vya jirani

Ofisa Uhifadhi wa Taifa Ruaha Kitengo cha Uhusiano kwa Jamii Priscus Mrosso akizungumza na Ofisa Mtendaji Kijiji cha Tungamalenga Linuss Mweluka kuhusu kuendelea kuimarisha mahusiano yao ya ujirani mwema kati yao,TANAPA na Hifadhi ya Taifa ya Ruaha,lakini pia kuhakikisha wanashiriki kulinda miradi mbalimbali inayoratibiwa na Hifadhi ikiwemo Elimu na Afya.PICHA ZOTE NA MICHUZI JR-RUAHA.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments