DC MBONEKO AKAGUA UTEKELEZAJI MRADI WA MAJI MWANDUTU, AWATAKA WANANCHI WAUNGANISHE MAJI MAJUMBANI MWAO

  Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Jasinta Mboneko, akiwa katika mji wa bwana Robert Mahizi mkazi wa kijiji cha Mwasekagi Kata ya Solwa wilayani Shinyanga ambaye amevuta maji nyumbani kwake na kumtua ndoo kichwani mke wake kwa kuchota maji akiwa nyumbani.


Na Marco Maduhu, SHINYANGA

MKUU wa wilaya ya Shinyanga Jasinta Mboneko, ametembelea katika kijiji cha Mwandutu Kata ya Solwa wilayani Shinyanga, ili kuona utekelezaji wa agizo lake la kutaka maji yatoke kwenye mradi wa kijiji hicho na kuhudumia wananchi.

Mboneko amefanya ziara hiyo leo Oktoba 4, 2022, katika kijiji cha Mwandutu kuona utekelezaji wa agizo lake ambalo alilitoa Septemba 7 mwaka huu kwenye mkutano wa hadhara alipofanya ziara kijijini humo na kuagiza mradi wa maji ukamilike haraka, ambao unatekelezwa na Wakala wa Majisafi na Usafi wa Mazingira vijijini (RUWASA) wilayani Shinyanga.

Akizungumza kwenye ziara hiyo amewapongeza RUWASA pamoja na Mkandarasi, kwa kutekeleza agizo lake na mradi huo wa maji kwa sasa umeanza kutoa huduma kwa wananchi.

“Rais wetu Samia Suluhu Hassan amekuwa akitoa fedha kwa ajili ya utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maendeleo, hivyo sisi wawakilishi wake lazima tuzisimamie fedha hizi ili zitekeleze malengo yaliyokusudiwa, na sasa mradi huu unatoa maji,” amesema Mboneko.

Aidha, amewataka wananchi wavute maji hayo majumbani mwao, ili waepukane kufuata huduma ya maji kwenye vituo na kutekeleza adhima ya Rais Samia ya kumtua ndoo kichwani mwanamke, huku akiwasihi wasitumie vishoka wakati wa uvutaji maji hayo bali wawatumie wataalam kutoka RUWASA.

Nao baadhi ya wananchi wa kijiji hicho akiwamo Rahel Rutonja, wameishukuru Serikali kwa kuwatekelezea mradi huo wa maji safi na salama kutoka Ziwa Victoria kijijini humo, ambapo awali walikuwa wakitumia maji ya kwenye visima na mabwawa ambayo siyo salama kiafya.

Kwa upande wake Kaimu Meneja Wakala wa Majisafi na Usafi wa Mazingira (RUWASA) wilayani Shinyanga Mhandisi Andrew Mogella, amesema mradi huo wa maji umekamilika kwa asilimia 98 na unatoa huduma ya maji, na vimebakia vitu vichache kuukamilisha ili uzinduliwe rasmi, na umegharimu Sh.milioni 305.

Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Jasinta Mboneko, akizungumza na wananchi wa kijiji cha Mwandutu Kata ya Solwa wilayani Shinyanga, alipotembelea kuona utekelezaji wa mradi wa maji kijijini humo, ambao umeshaanza kutoa huduma kwa wananchi.

Diwani wa Solwa Awadhi Mbaruku akizungumza kwenye ziara hiyo ya Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Jasinta Mboneko katika kijiji cha Mwandutu.

Kaimu Meneja Wakala wa Majisafi na Usafi wa Mazingira (RUWASA) wilayani Shinyanga Mhandisi Andrew Mogella, akieelezea utekelezaji wa mradi huo wa maji ya Ziwa Victoria katika kijiji cha Mwandutu.

Mwananchi Rahel Rutoja, akiipongeza Serikali kwa kuwatekelezea mradi huo wa Majisafi na salama kutoka Ziwa Victoria kijijini humo.

Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Jasinta Mboneko, akifungua maji kwenye mradi wa maji katika kijiji cha Mwandutu Kaya ya Solwa wilayani Shinyanga na kujiridhisha kuanza kutoa huduma kwa wananchi.

Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Jasinta Mboneko, akibeba ndoo ya maji katika mradi wa maji katika kijiji cha Mwandutu Kata ya Solwa wilayani Shinyanga.

Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Jasinta Mboneko akimtwisha ndoo ya maji mwananchi Matha Cherehani mkazi wa kijiji cha Mwandutu alipofanya ziara kuona utekelezaji wa mradi wa maji kijijini humo ambao umeanza kutoa huduma kwa wananchi.

Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Jasinta Mboneko akimtwisha ndoo ya maji mwananchi Rahel Rutonja mkazi wa kijiji cha Mwandutu alipofanya ziara kuona utekelezaji wa mradi wa maji kijijini humo ambao umeanza kutoa huduma kwa wananchi.

Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Jasinta Mboneko, akiwa katika mji wa bwana Robert Mahizi ambaye amevuta maji nyumbani kwake na kumtua ndoo kichwani mkewake na kuchota maji akiwa hapo hapo nyumbani.
Wananchi wa kijiji cha Mwandutu akichota maji.

Awali wanawake wa kijiji cha Mwandutu Kata ya Solwa wilayani, Shinyanga wakimpokea Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Jasinta Mboneko kwa furaha alipofika kijijini humo kuona utekelezaji wa agizo lake la mradi wa maji kuanza kutoa huduma hiyo haraka kwa wananchi.

Awali Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Jasinta Mboneko, akiwasili katika kijiji cha Mwandutu kuona utekelezaji wa mradi wa maji kijijini humo ambao umeshaanza kutoa huduma kwa wananchi.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments