WATU SABA WAFARIKI KWA KIMBUNGA KOREA KUSINI

WATU saba nchini Korea Kusini wamefariki dunia baada ya kukwama katika eneo la maegesho ya magari chini ya ardhi wakati wa mafuriko yaliyosababishwa na kimbunga Hinnamnor. Walikuwa wameshuka ili kusogeza magari yao lakini walishindwa kutoka katika maegesho hayo baada ya maji kujaa.

Kikosi cha waokoaji kilisema waliwaokoa watu wawili, ambao inasemekana walinusurika kwa kung’ang’ania mabomba ya dari kwa zaidi ya masaa 12. Kimbunga Hinnamnor, kimbunga kikali zaidi mwaka huu hadi sasa, kiliikumba Korea Kusini mapema wiki hii.


Kulingana na tovuti ya habari ya Yonhap, watu wote tisa walikuwa wakazi wa jengo la ghorofa ambao mapema Jumanne asubuhi walikuwa wameambiwa na ofisi ya usimamizi kuhamisha magari yao kutoka kwa maegesho.

Walionusurika – mwanamume mwenye umri wa miaka 30 na mwanamke mwenye umri wa miaka 50 – wanasemekana kuwa katika hali nzuri.
Watu wawili wameripotiwa kuokolewa

Pohang, jiji ambalo janga hilo lilitokea, lilipata uharibifu mbaya zaidi kote nchini, alisema Rais Yoon Suk-yeol. Bw Yoon alielezea masikitiko yake juu ya kuzama kwa maji, na kuyataja kuwa “maafa”. “Huko Pohang, wakazi walikwenda kuchukua magari yao … lakini walipatwa na maafa kama hayo, sikuweza kulala usiku” alisema Rais.


Takriban watu 10 sasa wamekufa kutokana na kimbunga Hinnamnor, kilichosomba pwani ya kusini na mashariki mwa Korea Kusini Jumatatu na Jumanne, kikiendesha mawimbi makubwa, upepo mkali na mvua kubwa.


Imeandikwa na Peter Nnally kwa msaada wa mitandao.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments