WALIOWACHAPA VIBOKO WAKULIMA USIMBE WAKAMATWA



_Na.Abel Paul wa Jeshi la Polisi,kibiti Pwani_

Jeshi la Polisi kwa kushirikiana na vyombo vingine vya ulinzi na usalama vimefanikiwa kuwatia mbaroni watuhumiwa saba wa matukio ya uchochezi wa migogoro baina ya wakulima na wafugaji katika kitongoji cha Usimbe kata ya Maparoni  tarafa ya Mbwera Wilaya ya Kibiti mkoa wa Pwani iliyotokea Agosti 30 mwaka huu.

Akitoa taarifa hiyo leo Septemba 10 2022 alipofika katika Kata ya Maparoni wilaya ya kibiti kamanda wa Polisi kikosi cha kuzuia wizi wa mifugo Nchini kamishina msaidizi wa Polisi ACP Simon Pasua amesema Jeshi la Polisi limefanikiwa kuwakamata watuhumiwa saba wa waliohusika katika tukio la kuwapiga wananchi wa Usimbe Kata ya Maparoni wilaya ya Kibiti mkoa wa Pwani.

Pasua amesema watuhumiwa hao bado wanashikiliwa na Jeshi hilo huku akisema kuwa majina yao yanahifadhiwa kwa sababu za kiupelelezi na kubainisha kuwa wamehojiwa na kukiri kufanya matukio hayo kama iliyoonekana katika video iliyosambaa katika baadhi ya mitandao ya kijamii.

Kamanda Pasua ameeleza kuwa  watuhumiwa wote watafikishiwa katika vyombo vya sheria pindi upelelezi utakapokamilika kujibu tuhuma zinazowakabili.

Sambamba na hilo ACP Pasua amewaeleza waandishi wahabari kuwa Jeshi la Polisi linawataka wale wote waliohusika katika tukio hilo baya  wajisalimishe katika vituo vyao Polisi kabla wajakumbana na mkono wa dola.

Hata hivyo ameongeza  kuwa kuna taarifa za baadhi ya wafugaji wanaohamisha mifugo kutoka eneo moja kwenda eneo jingine kwa lengo la kutafuta malisho ambapo amesema vitendo hivyo vimekuwa chanzo cha migogoro ya wakulima na wafugaji katika maeneo mengi hapa nchini ambapo amewataka kufuata matumizi bora ya ardhi.
 
Naye diwani wa kata Maparoni katika wilaya ya Kibiti ameliomba Jeshi la Polisi hususani kikosi kinachoshughulika na migogoro ya wakulima na wafugaji kuongeza kasi ya kuwatafuta watuhumiwa wengine waliohusika katika tukio hilo.

Abel Paul
Afisa habari wa Jeshi la Polisi 
0759783894

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments