KAMPUNI YA TEKNOLOJIA YA UCHAGUZI YAGOMA KUMFUNGULIA SEVA RAILA ODINGA


Kampuni iliYotoa teknolojia ya kupigia kura kwa tume ya uchaguzi ya IEBC nchini Kenya imekataa kufungua seva za kituo kikuu cha kitaifa cha kuhesabia kura kutokana na masuala ya usalama.


Katika barua iliyoandikia pande husika za kesi ya kupinga uchaguzi inayoendelea katika mahakama ya juu , kampuni hiyo kwa jina Smartmatic International Holdingn B.V imesema kwamba ufunguzi wa mfumo huo uliotumika kupeperusha matokeo ya fomu 34C utakiuka haki zake za kimsingi.

Barua hiyo iliyoandikwa tarehe 31 mwezi Agosti 2022, ilijiri kufuatia tofauti iliyoibuka kati ya walalamishi wanaopinga uchaguzi wa Urais na tume ya Uchaguzi IEBC kuhusu kuingia katika seva hizo ili kuchunguza kilichopo ndani yake.

Wakili Phillip Murgor siku ya Alhamisi alilalamika mbele ya mahakama kwamba IEBC ilikataa kuheshimu agizo la mahakama kwa kuwanyima maafisa wake fursa ya kuingia na kufanya uchunguzi katika seva zote nane.

"IEBC ilikataa seva zake kuchunguzwa . Walituruhusu kuchunguza seva tano pekee na tukaona kiwango kikubwa cha ufutaji wa data muhimu na kwasababu muda unayoyoma watatupatia habari zisizo muhimu’’, alisema Murgor.

Katika barua hiyo kampuni ya Smartmatica inaongezea kwamba kumfungulia seva hizo mlalamishi kutafanya mfumo huo kutokuwa salama kwa sababu huenda ukatumika katika chaguzi zijazo nchini Kenya au kwengineko duniani.

''Mbali na kukiuka haki za kimsingi za kampuni hiyo , hatua hiyo pia itahatarisha uchaguzi katika maeneo mengine ambayo yanatumia ama yamewahi kutumia mfumo wetu'', kampuni hiyo ilisema.

Hata hivyo mahakama ilisema kwamba tayari imepokea ripoti kuhusu uchunguzi wa seva hizo siku ya Jumatano jioni na kuwataka mawakili kuandaa malalamishi yao kuhusu suala hilo wakati watakapohitajika kufika mbele ya mahakama hiyo.

Chanzo - BBC SWAHILI

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments