UGANDA YATHIBITISHA MLIPUKO WA EBOLA...MTU MMOJA AFARIKI

Mwanaume mwenye umri wa miaka 24 aliyeambukizwa Ebola amefariki dunia katikati mwa Uganda katika mlipuko mpya uliothibitishwa na maafisa wa afya.

Waziri wa afya amewaambia waandishi wa habari kwamba mwathiriwa alikuwa ameonyesha dalili kabla ya kuugua ugonjwa huo.

Alikuwa mkazi wa kijiji cha Ngabano katika wilaya ya Mubende, yapata kilomita 147 (maili 91) kutoka mji mkuu, Kampala.


Kisa cha aina hiyo ambacho ni nadra kilithibitishwa na Taasisi ya Utafiti wa Virusi vya Uganda, Shirika la Afya Duniani (WHO) lilisema katika taarifa.

“Shukrani kwa utaalamu wake [Uganda], hatua imechukuliwa ili kubaini virusi hivyo haraka na tunaweza kutumia ujuzi huu ili kukomesha kuenea kwa maambukizi,’’ alisema Dk. Matshidiso Moeti - Mkurugenzi wa WHO kanda ya Afrika.

Shirika la Afya Ulimwenguni linasema kuwa ni mara ya kwanza katika kipindi cha takriban muongo mmoja kwa kesi ya Ebola kuthibitishwa nchini humo.

Takriban watu wanane walio na dalili zinazoshukiwa wanapokea huduma ya matibabu, na WHO sasa inatuma wafanyikazi katika eneo lililoathiriwa.

Visa vingi vya virusi hivyo vimeripotiwa katika nchi jirani ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, hivi karibuni zaidi ikiwa mwezi uliopita.

Sampuli zilizokusanywa kutoka kwa mwanamume huyo ambaye aliwasilishwa hospitalini akiwa na dalili za maambukizi ya virusi vilipatikana na virusi vya ugonjwa wa Ebola aina ya Sudan.

Kijana huyo alikuwa mgonjwa kwa takriban siku nne, na amekufa.

Baada ya uchunguzi wa maafisa wa afya, vifo vingine sita katika familia moja vimethibitishwa kuwa Ebola.

Wizara ya afya nchini Uganda imedhibitisha watu sita wamefariki wilayani Mubende wakiwa na dalili za ugonjwa wa Ebola.

Watu wazima watatu na watoto watatu walikufa katika hali isiyoeleweka ndani ya wiki mbili zilizopita.

Marehemu ni pamoja ni pamoja na mtoto wa kike wa miezi 10 ambaye alifariki tarehe 11 Septemba 2022.

Inasemekana kuwa walionyesha dalili za Ebola.

Timu za afya ya jamii sasa zinafuatilia watu wowote ambao wanafamilia wanaweza kuwa wamewasiliana nao.

Familia hizi zitatengwa na kuwekwa chini ya karantini.

Wizara ya afya ya Uganda ilisema kuwa chanjo pekee zinazopatikana nchini humo ni zile zilizokusudiwa kwa aina ya Ebola ya Congo.

Lakini mamlaka imewahakikishia umma kuwa wana uwezo na ujuzi wa kudhibiti Ebola, kulingana na uzoefu wa awali wa milipuko ya virusi.

Shirika la Afya Ulimwenguni pia linatuma wafanyikazi wa ziada kwenye eneo lililoathiriwa.

Hii ni mara ya tano Uganda kupata mlipuko wa ugonjwa wa Ebola, mara ya kwanza ulikuwa mbaya zaidi mwaka 2000 na kuua watu 224, na mlipuko wa mwisho nchini ilikuwa mwaka 2018. Milipuko mingine ilitokea 2014 na 2017.

CHANZO - BBC SWAHILI

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments