MKOA WA KATAVI UMEFANIKIWA KUYAFIKIA MAENEO YOTE TA WATU WALIOTAKIWA KUHESABIWA


Mkuu wa Mkoa wa Katavi Mwanamvua Mrindoko akiwa anahesabiwa na Karani wa sensa wa eneo Namba 002 Astoni Kajiba katika mtaa wa Ilembo manispaa ya Mpanda nyumbani kwake kwenye zoezi la sensa ya watu na makazi lililoanza tarehe 23.
Mkuu wa Mkoa wa Katavi Mwanamvua Mrindoko akiwa katika Mtaa wa Mpanda Hoteli nyumbani kwa Mzee Alikado Mwima wakati akiwa anatembelea kaya mbambali za wananchi wa Mkoa wa Katavi wakati alipokuwa akikagua maendeleo ya zoezi la sensa linavyoendelea kufanyika Mkoani Katavi katika siku ya kwanza ya zoezi la sensa ya watu na makazi linaloendelea Mkoani hapa na limefanyika kwa ufanisi mkubwa. picha na Walter Mguluchuma

Na Walter Mguluchuma - Katavi.

Mkoa wa Katavi umefanikiwa kuyafikia maeneo yote ya muhimu kwa wakati ambayo watu walitakiwa kuhesabiwa kuanzia saa sita na dakika moja usiku yakiwepo maeneo ya stendi zote za nyumba za kulala wageni ,baa, Hospitalini, magereza, watoto wa mitaani na kwenye treni ya abiria inayofanya safari ya kutoka Mpanda kwenda Tabora.


Pia kwenye zoezi hilo la Sensa ya watu na Makazi linaloendelea kufanyika mkoani Katavi hadi sasa hakuna changamoto yoyote ambayo imeishajitokeza na wananchi wamehamasika sana na wanatoa ushirikiano mkubwa kwa makarani wa sensa .


Akizungumza na waandishi wa Habari mbele ya wananchi wa Mkoa wa Katavi Mwanamvua Mrindoko kwenye maeneo mbalimbali aliyokuwa akiyatembelea katika Manispaa ya Mpanda wakati akikagua maendeleo ya zoezi la sensa alisema kuwa maeneo yote ya muhimu yameweza kufikiwa kwenye zoezi la sensa kwa wakati na na bila kuwepo kwa changamoto yoyote ile hadi sasa.


Amebainisha kuwa wananchi wa Mkoa wa Katavi wamehamasika  kwenye zoezi hilo na wako tayari kuhesabiwa ambapo kwenye zoezi hili wananchi wamekuwa wakitoa ushirikiano mkubwa huku hali ya maeneo yote ni salama.

Mrindoko alisema kuwa kwenye zoezi hilo wanahakikisha linafanikiwa kwa asilimia mia moja na watu wote wanafikiwa na kuhesabiwa kama ilivyokusudiwa bila kujali hali ya jiografia ya Mkoa ilivyo.


Katibu Tawala wa Mkoa wa Katavi Haasan Abasi Rugwa amesema kuwa zoezi hili katika Mkoa wa Katavi limeanza kwa ufanisi mkubwa huku ulinzi na usalama ukiwa umeimarika na mpaka sasa hakuna malalamiko yoyote ya kutoka kwa wananchi kutokana kazi kubwa ambayo imefanywa ya zoezi la sensa kwenye Mkoa wa Katavi.

Hivyo amewataka kila wananchi wa Mkoa wa Katavi kuhakikisha anahesabiwa na ndiyo mkakati ambao Mkoa umejiwekea wa kuhakikisha hakuna mtu hata mmoja ambaye hatahesabiwa kwenye zoezi hili .


Karani wa Senza wa eneo namba 002 huko katika eneo la Ilembo Aston Kajiba amesema kuwa zoezi hilo kwa upande wake limekuwa likienda vizuri kutokana na ushirikiano kutoka kwa wana wananchi kwani kila Kaya ambayo amekuwa akiifikia amekuwa amekuta wakiwa tayari wameandaa nyaraka muhimu zinazo hitajika kwenye zoezi hilo hali ambayo inaonyesha kuwa watu wamekuwa na uwelewa wa umuhimu wa sensa ya watu na makazi

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments