GGML WATOA MAGODORO 50 KWA KITUO CHA WAZEE BUKUMBI

Afisa Mwandamizi wa Mahusiano ya Jamii kutoka GGML, Shunashu Musa (kulia) akimkabidhi magodoro 50 msimamizi wa Kituo cha Wazee Bukumbi, Jonas Tarimo. Anayetazama ni Afisa Mahusiano wa Jamii wa GGML, Fredrick Musa (wa kwanza kulia).
Sehemu ya wazee wa Kituo cha Wazee cha Bukumbi wakisubiri msaada wa GGML.

Na Mwandishi wetu - Mwanza

KATIKA kuunga mkono juhudi za Serikali kuwajali na kuboresha maisha ya wazee nchini, Kampuni ya Uchimbaji Madini ya Dhahabu Geita (GGML) imetoa msaada wa magodoro 50 kwa Kituo cha Wazee Bukumbi kilichopo mkoani Mwanza.


Akizungumza katika hafla ya kukabidhi msaada huo jana mkoani Mwanza, Ofisa Mwandamizi wa Mahusiano ya Jamii kutoka GGML, Shunashu Musa alieleza kuwa msaada huo unalenga kuboresha makazi bora na hali ya maisha ya wazee wanaoishi katika kituo hicho.


Aliongeza kuwa baadhi ya wafanyakazi wa GGML na wenzao wamekuwa wakisaidia kituo hicho kwa nyakati tofauti na kuchangia baadhi ya vifaa vya matumizi. Kipindi hiki menejimenti ya kampuni hiyo imeamua kusaidia kituo hicho kwa kuchangia uboreshaji wa vyumba vya kulala vya wazee hao.


“Tulipokea ombi la kufikiria kusaidia kituo hiki kwa njia mbalimbali. Tunafahamu kituo hicho kilianzishwa miaka mingi iliyopita hivyo baadhi ya miundombinu na vifaa vinahitaji maboresho ndiyo maana uongozi uliamua kuchangia magodoro 50.

"Kama sehemu ya AngloGold Ashanti, moja ya maadili ya biashara ya GGML ni kwamba jumuiya na jamii tunakofanyia kazi lazima ziwe na maisha bora. Tunatumaini magodoro haya yataboresha maisha ya wazee zaidi ya 50 wanaoishi hapa,” alisema.



Aidha, Msimamizi wa Kituo cha Wazee cha Bukumbi, Jonas Tarimo alishukuru GGML kwa msaada huo na kuongeza kuwa utasaidia kutoa huduma za malazi bora na salama kwa wazee wa kituo hicho.



“Hiki ndicho kituo pekee cha kuishi wazee kilichopo karibu na mikoa ya Geita na Mwanza. Tumebahatika kuungwa mkono na Mgodi wa Dhahabu wa Geita ndio maana tunaona wakazi wengi wanafurahia msaada huu,” alisema.


GGML imekuwa kinara wa uwekezaji katika jamii tangu ilipoanzishwa mwaka 2000, huku vipaumbele vikubwa vikiwa ni miradi ya afya, elimu, maji, barabara, miradi ya maendeleo na miradi mingine ya kijamii inayolenga kuboresha ustawi wa jamii inayowapokea.


Mapema mwaka huu, Kampuni ilitangazwa kuwa mshindi wa jumla wa makampuni yaliyofanya vyema katika sekta ya madini nchini Tanzania kwa mwaka wa 2020/2021 baada ya kushinda tuzo za uwajibikaji wa kampuni kwa jamii, mazingira, usalama, mlipakodi bora na maudhui ya ndani.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments