WANAUME WATAKIWA KUANZISHA MAJUKWAA KUWALINDA WATOTO

Waziri wa Maendeleo ya Jamii,Jinsia,Wanawake na Makundi maalumu Dkt.Dorothy Gwajima  akizungumza leo June 16,2022 Jijini Dodoma katika kilele cha siku ya Mtoto wa Afrika . 

Mbunge wa Morogoro vijijini Hamis Shaban Taletale (Babu tale) .

Na Dotto Kwilasa,DODOMA 

WANAUME nchini wametakiwa kuanzisha majukwaa ya kuwasemea watoto dhidi ya ukatili wa kijinsia hali inayotajwa kuleta usawa na kuwaelimisha wanaume wengine kuheshimu haki za msingi za watoto ikiwemo Usalama wao mtandoni ,elimu ,afya na kulindwa. 

Waziri wa Maendeleo ya Jamii,Jinsia,Wanawake na Makundi maalumu Dkt.Dorothy Gwajima amesema hayo leo June 16,2022 Jijini Dodoma wakati akizungumza katika kilele cha siku ya Mtoto wa Afrika kilicho ambatana na uzinduzi wa Mwongozo wa Taifa wa uanzishaji na uendeshaji wa Mabaraza ya Watoto na Mwongozo wa Taifa wa Dawati la Ulinzi na Usalama wa Mtoto Ndani na Nje ya Shule.

Pamoja na jitihada mbalimbali za kukabiliana na vitendo vya ukatili kwa watoto,Dkt.Gwajima amesema  bado juhudi hizo hazijazaa matunda na kuzidi kuongezeka siku hadi siku huku watuhumiwa wakuu wa Matukio hayo wakiwa ni wanaume. 

 Amesema pamoja na watuhumiwa hao wa ukatili kuchukuliwa hatua kali za kisheria, bado ongezeko la taarifa za vitendo vya ukatili wa aina mbalimbali vinaongezeka ikiwemo Ubakaji, Ulawiti, Utumikishwaji wa watoto katika ajira hatarishi, Ukeketaji, Ndoa na mimba za utotoni na vitendo vingine vya ukatili. 

 "Nadhani Sasa ifike wakati na nyinyi wanaume mtusaidie kulikemea suala hili Kwa vitendo maana ukisikia mtoto amebakwa mwanaume ndo anahusika,mtoto akiwa na mimba ni mwanaume anahusika,akilawitiwa mwanaume pia anahusika,sasa kwanini na nyie msianze kuwakemea wanaume wenzenu ili waache hii tabia;!lihoji Dkt.Gwajima.

 Amesema ikiwa wanaume wataanzisha majukwaa mbalimbali na kuyatumia ipasavyo kuwafundisha watoto ishara zote za ukatili,hali hiyo itapungua na kuongeza nguvu ya matumaini kwa wanaharakati wengine. 

 "Kuna watoto wanakatiliwa lakini hawajijui,hebu tusaidieni hili ili wajue mtu anapomuita na kumpa pipi na biskuti ni kiashiria cha kutaka kumbaka au kumlawiti,tuwafundishe watoto wetu wakatae rifti,wakatae kuitwa na watu wasiowajua ,"amesema 

 Sambamba na hayo Dkt.Gwajima ameitaja Mikoa vinara iliyoongoza kwa vitendo vya ukatili wa watoto kuwa ni Arusha (808), Tanga (691), Shinyanga (505), Mwanza (500) na Mkoa wa Kipolisi Ilala (489) huku makosa yaliyoongoza kwa idadi kubwa yakiwa ni ubakaji (5,899), mimba kwa wanafunzi (1,677) na ulawiti (1,114) 

 Ameeleza kuwa tayari Serikali kupitia Wizara yake imeanzisha Mpango kazi wa Taifa wa kupambana na vitendo vya ukatili dhidi watoto vinavyofanyika mtandaoni na kuandaa machapisho au majarida ya kufundishia Watoto, Wazazi na Walimu kuhusu ukatili wa Watoto mtandaoni.

 Kutokana na hayo ,Mbunge wa Morogoro vijijini Hamis Shaban Taletale (Babu tale) amesema anajitolea kuwa balozi wa kupinga ukatili wa kijinsia kwa watoto kwa kutumia jukwaa la mitandao ya kijamii ili kila mwanaume anaye jihusisha na vitendo hivyo ajifunze na kujutia makosa yake. 

 "Mimi ni Mbunge,nitatumia nafasi yangu kuelimisha wanaume wenzangu kupitia  akaunti zangu za mitandao ya kijamii kama jukwaa la kuelimisha ,nina watu wengi wanaofuatilia  ambapo kila mtandao una zaidi ya watu milioni tatu,nitatumia nafasi yangu kuelimisha wanaume wenzangu kuachana na tabia chafu ya ulawiti,ubakaji na nyinginezo,"amesema na kuongeza 

 "Na kwa vile mimi ni baba ninaye walea watoto wangu wawili mwenyewe,ninajua uchungu wa mtoto,hivyo Mheshimiwa Waziri naomba nitangaze rasmi kupitia jukwaa hili kwamba kuanzia leo mimi ni balozi wa kupinga ukatili kwa watoto, nitahakikisha kila ninapopata nafasi nalikemea hili,"anasisitiza Taletale 

 Pamoja na hayo Mbunge huyo amesema jamii inapaswa kuwa na uchungu na kuwachukulia watoto wa mwenzao kama wakwao. 

 "Mtoto wa mwenzio ni wako,maana yangu ni kwamba kila mtoto anastahili kupendwa na kuthaminiwa,sisi tusipowakemea wanaowakatili watoto hali hiyo itaendelea niwashauri tu wazazi wenzangu tuwajengee watoto mazoea ya kuwa na utayari wa kutokaa kimya wanapotendewa ukatili,"amesisitiza 

 Chimbuko la Siku ya Mtoto wa Afrika limetokana na azimio la Umoja wa nchi za Afrika (OAU) la mwaka 1991 lililokuwa na lengo la kuwaenzi Watoto kutoka shule mbalimbali za nchini Afrika Kusini hususani Kitongoji cha Soweto waliouawa kinyama na Polisi wa Serikali ya Makaburu tarehe 16 Juni,1976. 

 Watoto hao wanaokadiriwa kufikia 2000 waliuawa wakati wanaandamana kupinga elimu ya kibaguzi dhidi ya watoto wenye asili ya kizungu wakiwa wanashinikiza elimu itolewe kwa usawa na kuzingatia lugha yao ya asili ili washiriki vema katika kupata elimu bora na kwamba toka kipindi hicho, maadhimisho haya yamekuwa yakitumika na Serikali na wadau katika nchi za Afrika kuelimisha na kuwakumbusha Wazazi, Walezi na jamii wajibu wao katika kuwapatia watoto haki zao za msingi zikiwa pamoja na Lishe bora, Malazi, Ulinzi, Elimu na Huduma za afya.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments