RC MAKALLA ATOA WITO KUSHIRIKI TAMASHA LA UTAMADUNI NA SIKU YA KISWAHILI DUNIANI

Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Mhe.Amos Makalla akizungumza na waandishi wa habari leo Juni 29,2022 katika Ofisi za Habari Maelezo JNICC Jijini Dar es Salaam
Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Mhe.Amos Makalla akizungumza na waandishi wa habari leo Juni 29,2022 katika Ofisi za Habari Maelezo JNICC Jijini Dar es Salaam. kushoto ni Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo Bw. Saidi Yakubu



***************************



- Rais Samia Mgeni rasmi Maadhimisho ya Siku ya Kiswahili Duniani Julai 07.

Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam Mhe. Amos Makalla ametoa wito kwa Wananchi kujitokeza kwa wingi kwenye Tamasha la Utamaduni la kwanza kitaifa na Siku ya Kiswahili Duniani linalotaraji kuanza July 01-07 Jijini humo na kuhudhuriwa na Viongozi mbalimbali akiwemo Rais Samia Suluhu Hassan.

Akizungumza na Waandishi wa habari, RC Makalla amesema Tamasha Hilo litazinduliwa Julai 02 na Waziri Mkuu Mhe. Kassim Majaliwa kwenye Uwanja wa Uhuru likihusisha Matembezi ya Utamaduni, Maonyesho ya vyakula vya asili na ngoma za asili.

Aidha RC Makalla amesema Julai 03 kutakuwa na Usiku wa Taarabu katika ufukwe wa Coco Beach ukihusisha burudani ya Mziki mwanana kutoka kwa wasanii mbalimbali akiwemo Khadija Kopa, Isha Mashauzi, Patricia Hilary, Mzee Yusuph na wasanii na vikundi ambapo Mgeni rasmi anatarajiwa kuwa Spika wa Bunge Dkt.Tulia Ackson.

Hata hivyo RC Makalla amesema Julai 04 Kutakuwa na maandamano ya Amani kuhusu Lugha ya Kiswahili na Utoaji haki kutoka Temeke mwisho mpaka Uwanja wa Uhuru ambapo Mgeni rasmi anatarajiwa kuwa Waziri wa Katiba na sheria Dkt. Damas Ndumbaro.

RC Makalla amesema Julai 06 kutakuwa na kongamano la mchango wa lugha ya Kiswahili katika harakati za ukombozi wa bara la Afrika likihusisha Viongozi kutoka ndani na nje ya Nchi.

Pamoja na hayo RC Makalla amesema Julai 07 Rais Samia Suluhu Hassan anatarajiwa kuwa mgeni rasmi kwenye Siku ya Kiswahili Duniani ambayo itaadhimishwa kwa mara ya kwanza Dunia Ambapo ametoa wito kwa Wananchi kujitokeza kwa wingi siku hiyo.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments